Raia wa Kigeni Waushika Uchumi wa Tanzania......Ni 10% Tu Ya Watanzania Wanaomiliki Uchumi wa Nchi, Serikali Yatangaza Mkakati Kuokoa Jahazi - LEKULE

Breaking

10 Feb 2016

Raia wa Kigeni Waushika Uchumi wa Tanzania......Ni 10% Tu Ya Watanzania Wanaomiliki Uchumi wa Nchi, Serikali Yatangaza Mkakati Kuokoa Jahazi



WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa, amesema serikali ya awamu ya tano inafanya kila juhudi kuhakikisha uchumi wake unamilikiwa na wananchi, nia ikiwa ni kuifanya nchi kuwa na uchumi wa kati.

Majaliwa aliyasema hayo jana, wakati akizindua mpango wa uwezeshaji wananchi kiuchumi, ambao pamoja na mambo mengine utatoka na mapendekezo ya nini cha kufanya kufikia malengo yake.

Kwa mujibu wa waziri mkuu, ili kufikia malengo ya mkakati huo, wadau wote hawana budi kuunganisha nguvu pamoja kuanzia ngazi ya juu hadi chini.

“Taarifa zilizopo zinaonyesha ni asilimia 10 tu ya Watanzania ndio wanaomiliki uchumi wa nchi na sera hiyo ndiyo inatoa mwongozo wa jumla unaohakikisha kwamba wananchi wanapata fursa mbalimbali za kiuchumi ambazo zitawawezesha kujenga na kufaidika na uchumi wa mchi yao,” alisema.
 
Aidha alizitaja mojawapo ya nyenzo muhimu katika kufanikisha suala hilo ni pamoja na uhakika wa masoko, riba nafuu kwa wajasiriamali, pamoja na ushirikishwaji wa viongozi wote.

“Napenda mkimaliza mkutano wenu mnipatie mapendekezo ya kile mlichokubaliana hapa, kwani nimekuwa na utaratibu kila nikifanya ziara zangu mikoani lazima nizungumze na wananchi na huwa nawaeleza haya masuala ya mipango ya serikali katika kuwawezesha,” alisema waziri mkuu.

Awali akimkaribisha waziri mkuu, Waziri wa Nchi Ofi si ya Waziri Mkuu Sera, Uratibu, Bunge, Uwezeshaji, Ulemavu Vijana na Wazee, Jenister Mhagama, alisema kuwa kuwawezesha wananchi ni hatua muhimu katika maendeleo ya taifa.
 
Katika kufanikisha azma hiyo, Waziri Jenister alisema tayari serikali imefanikiwa kutenga maeneo maalumu ya uwekezaji, ambapo vijana na wananchi kwa ujumla watapewa kipaumbele zaidi.

“Mikoa 20 tayari imeshatenga maeneo na sasa wanaweka miundombinu ambayo nia yake ni kuwasaidia wananchi kuweza kumiliki uchumi wao,”alisema.

Hatahivyo mojawapo ya changamoto inayokabili utekelezaji wa sera ya uwezeshaji wananchi kiuchumi ni ukosefu wa ajira na umasikini, ambavyo vinalikabili kundi hili muhimu.

Imeelezwa kuwa maeneo ambayo yanatajwa kama sehemu muhimu zenye kuwezesha kupatikana kwa matokeo ya haraka ni sekta ya utalii, ujenzi, usafirishaji, kilimo, madini, misitu na viwanda

No comments: