Mramba Afunguka Kuhusu Maisha Ya Gerezani.....Aishauri Serikali Kuwatumia Wafungwa Wenye Utaalumu Badala Ya Kuwarundika Gerezani - LEKULE

Breaking

10 Feb 2016

Mramba Afunguka Kuhusu Maisha Ya Gerezani.....Aishauri Serikali Kuwatumia Wafungwa Wenye Utaalumu Badala Ya Kuwarundika Gerezani



Aliyekuwa  Waziri wa Fedha katika Serikali ya awamu ya tatu, Basil Mramba, ameishauri Serikali kuhakikisha inawatumia wafungwa kutumikia jamii badala ya kuwarundika magerezani.

Amesema pamoja na hayo, maisha ya gerezani si salama na si njia pekee ya kumrekebisha mhalifu aliyehukumiwa na mahakama.

Kutokana na hali hiyo, alisema kuna haja kwa Serikali kuanza kutumia sheria namba 6 ya huduma kwa jamii kuwaangalia wafungwa wenye taaluma kutumika adhabu zao katika fani au taasisi za umma ili kupunguza gharama kuwahudumia watu ambao wanaweza kuisaidia jamii.

Mramba alitoa kauli hiyo jana, wakati yeye na mwenzake aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona, walipomaliza kufanya usafi katika Hospitali ya Sinza Palestina, Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kutumikia adhabu ya kifungo chao cha nje baada ya wiki iliyopita Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuridhia kuwa wanastahili kutumikia jamii kwa kipindi cha miezi sita hadi Novemba 5.

Alisema imekuwa ni kawaida jamii kuwa na mtazamo kwamba mtu yeyote anayekutwa na hatia lazima atapelekwa jela ajirekebishe na kuacha tabia aliyonayo jambo ambalo si sahihi.

“Jamii inaamini jela ni sehemu salama na mtu akishikwa na hatia kwa kosa lolote, mahala sahihi ni jela tu, kule anakutana na watu wa kila aina, wenye makosa tofauti, hali ambayo inamfanya ajifunze mambo mengine mapya.

“Unakuta mtu amefanya uhalifu wa kuiba kitu, anafungwa na kupelekwa gerezani, anakutana na majambazi sugu wanaompa mbinu zaidi, sasa akitoka jela anakuja akiwa ameiva, anarudia kwenye matukio akiwa amekamilika,” alisema Mramba.

Alisema kuwapeleka wafungwa katika huduma za kijamii kutasaidia kupunguza gharama kwa Serikali na msongamano ndani ya magereza.

Akizungumzia suala la kuwatumia wafungwa ambao ni wanataaluma, Mramba alisema sheria hiyo ikitumika vizuri italisaidia taifa kwani wapo baadhi ya wafungwa wana taaluma ya udaktari, ualimu, ufundi na uhasibu, ambao wanaweza kutumika katika fani zao kwenye taasisi za umma.

“Kuna maeneo mengine yana uhaba wa wataalamu ambao wengine wapo magerezani wanahudumiwa na Serikali kuanzia chakula, malazi na hata afya zao, hivyo wakiwatumia hao itakuwa faida kwa taifa kwa kuwa watafanya kazi bila malipo,” alisema Mramba.

Alisema suala la kuwatumia wafungwa katika huduma za kijamii si geni kwa nchi zilizoendelea ambako kwa kiasi kikubwa wamesaidia kuinua uchumi wa nchi zao.

Kwa siku ya jana, Mramba na Yona walianza kufanya usafi saa 2 asubuhi kwa kufagia nyuma ya jengo la wazazi katika hospitali hiyo.

Naye Ofisa Huduma za Jamii Mkoa wa Dar es Salaam, Deogratius Shirima, alisema gharama zinazotumika kuwahudumia wafungwa magerezani ni kubwa, hivyo ni vyema wale wanaoguswa na sheria ya huduma za jamii namba 6 ya mwaka 2002 kutumikia kifungo cha nje.

“Sheria hii ni vyema ikatumika kwa wale inaowagusa kwani itapunguza gharama za kuwahudumia magerezani, na pia adhabu wanayopata wafungwa wa nje ni wazi jamii ambayo ndiyo iliyokosewa inaona utekelezaji wake kwa uwazi,” alisema Shirima.

Alisema mataifa mengine ikiwamo nchi ya Kenya wanatumia sheria hiyo ambapo nusu ya wafungwa nchini humo wapo katika huduma za jamii.

Februari 6, mwaka huu mawaziri hao walibadilishiwa adhabu ya jela na kupewa adhabu ya kutumikia kifungo cha nje mwishoni mwa wiki iliyopita na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, baada ya kukamilika kwa mchakato wa kufikia hatua hiyo.

Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Cyprian Mkeha, alisema sheria ya huduma kwa jamii namba 6 kifungu namba 3(1) ya mwaka 2002 inasema mtu yeyote anayetiwa hatiani kwa kosa ambalo adhabu yake ni miaka mitatu kushuka chini mahakama inaweza kumpa adhabu ya kutumikia jamii.

Mramba na Yona, ambao baada ya rufaa walibakiwa na adhabu ya miaka miwili, walitiwa hatiani kwa kutumia madaraka vibaya ambapo walitakiwa kumaliza kifungo Novemba mwaka huu.

Hata hivyo, hakimu huyo alisema magereza walifikisha barua mahakamani hapo Desemba 5, mwaka jana yenye kumbukumbu namba 151/DAR/3/11/223, wakipendekeza kifungo cha nje kwa mawaziri hao.

Hakimu Mkeha alisema baada ya kupokea barua hiyo, mahakama iliamuru watu wa huduma za jamii kuchunguza kama wanastahili kupewa adhabu hiyo na kwamba walifanya hivyo na kurudisha ripoti kwamba wanastahili.

Alivitaja vigezo vya kupewa adhabu hiyo kuwa ni umri ambapo Mramba na Yona wana miaka 75.

No comments: