Waziri Magheme Atema Cheche.......Asema Waliomuita 'Waziri Mzigo' Wataisoma Namba - LEKULE

Breaking

29 Dec 2015

Waziri Magheme Atema Cheche.......Asema Waliomuita 'Waziri Mzigo' Wataisoma Namba


Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe, aliyeapishwa jana kushika wadhifa huo na Rais Dk. John Magufuli, amefunguka na kueleza sababu za kuitwa Waziri ‘mzigo’ wakati akiwa Wizara ya Maji, akitokea Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika.

Novemba 24,mwaka 2013, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, akiwa kwenye ziara za kuimarisha na kukagua Ilani ya chama hicho mkoani Ruvuma, kabla ya kuanza kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, alikutana na malalamiko ya wananchi juu ya uzembe wa mawaziri waliokuwa kwenye Serikali ya Rais Jakaya Kikwete, waliowaita ‘mizigo’.

Mawaziri wengine waliotajwa kuwa mizigo ni Dk. Shukuru Kawambwa (Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi), Christropher Chiza (Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika) na Naibu wake

Akijibu tuhuma hizo baada ya kupenya kwenye Baraza la Mawaziri la Rais Dk. Magufuli, tofauti na watu wengi walivyodhani kutokana kashfa hiyo, Profesa Maghembe alisema waliomtaja kuwa ni mzigo ni majangili waliokuwa wanawinda wanyama na waandishi waliokuwa wanaandika na kulipwa na majangili.
 
“Wanaosema Waziri Maghembe ni mzigo hawajui na hawajafanya utafiti na usipofanya utafiti, huna haki ya kuzungumza, na wafikishieni taarifa Maghembe amerudi tena,” alisema.

Alisema amejipanga kuhakikisha anapambana na ujangili nchini na kuongeza pato la taifa kupitia sekta hiyo.
 
Alisema atahakikisha wizara hiyo inaenda vizuri na rasilimali zilizopo zinalindwa ili zilifaidishe taifa.
 
“Jambo la kwanza nitakalolifanya ni kupambana na ujangili na tunawatumia salamu majangili wote kokote walipo, kiama chao kimefika…kwa sasa wakae nyumbani watafute shughuli za kufanya,” alisema.
 
Alitaja jambo la pili atakalolifanya katika sekta hiyo ni kuhakikisha misitu inatunzwa na kudhibiti watu wote wanaokata miti na kuchoma mkaa.
 
“Tutahakikisha mkaa utakaokuwa unachomwa ni ule wa lazima na siyo kuchoma hovyo. Hivyo tutaangalia namna ya kurahisisha nishati zilizopo ili kupunguza matumizi ya mkaa,” alisema.
 
Prof. Magembe alisema jambo la tatu ni kuhamasisha utalii na kuongeza idadi ya watalii kutoka nje kutoka milioni 1.2 hadi kufikia milioni tatu katika kipindi cha miaka mitatu.
 
“Hii ni sekta muhimu na ili kuongeza idadi ya watalii kufikia milioni mbili hadi tatu kwa kipindi cha miaka miwili ama mitatu ijayo ni lazima kuhamasisha,”alisema.
Alisema mwaka 2007 akiwa Wizara ya Maliasili na Utalii, katika kipindi hicho, alifanya kazi kubwa ya kuhakikisha katika sekta ya uwindaji wanaongeza mapato ya serikali kuanzia Dola milioni saba zilizokuwa zinapatikana hadi kufikia Dola milioni 70 na kwa msingi huo, yeye siyo mzigo.

Alisema pia walikuwa wakifanya kazi ya kukamata watu wanaosafirisha magogo kwenda nje ya nchi na kuongeza pato la taifa katika sekta ya misitu.


“Nashangaa hawa wanaoniita mimi ni mzigo, ningewezaje kufanya kazi hizi,” alisema Profesa Maghembe.

No comments: