NSSF Yapigwa Marufuku Ujenzi wa Miradi Mipya - LEKULE

Breaking

7 Apr 2016

NSSF Yapigwa Marufuku Ujenzi wa Miradi Mipya


Bunge limesimamisha utekelezaji wa miradi yote mipya ya Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) mpaka hapo Kamati na Wizara itakapopitia taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali (CAG), sambamba na kuitisha taarifa za utekelezaji wa miradi yote iliyofanywa na mifuko ya hifadhi ya jamii nchini.

Aidha, imeagiza ukaguzi wa kina wa ujenzi wa jengo jipya la Ofisi za Makamu wa Rais kwa kuangalia usalama wa jengo, hesabu zilizotumika kama zinaendana na thamani ya jengo na kama washauri walitoa ushauri wao ipasavyo.

Akizungumza katika kuhitimisha ukaguzi wa miradi mbalimbali ya serikali iliyofanywa na Kamati ya Katiba na Sheria, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mohamed Mchengerwa alisema NSSF ilitoa taarifa ya utekelezaji wa miradi ikiwa haijitoshelezi kwa kutoonesha gharama zilizotumika mpaka sasa, bajeti iliyopangwa kutumiwa na kiasi kilichosalia ili kubaini kama fedha zilizotumika zinalingana na thamani ya ujenzi wenyewe.

Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria kwa takribani siku tano kuanzia Machi 29, mwaka huu, ilitembelea Wizara ya Katiba na Sheria, Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu na Mahakama.

Akizungumzia taarifa za utekelezaji wa miradi iliyofanywa na mifuko yote ya hifadhi za jamii, Mchegerwa alisema kamati yake inataka kupitia taarifa zote za utekelezaji wa miradi sambamba na kupitia sera ya uwekezaji ili kuangalia kama yamefuata taratibu na hakuna upotoshaji.

“Kwanza kuna madeni makubwa ambayo mifuko hiyo inadai kwa wapangaji wao. Pia tunaangalia sera ya uwekezaji ili kujiridhisha kama ushauri wa kitaalamu uliotolewa unakidhi matakwa ya ujenzi unaoendelea.


Aliongeza: “Kuna majengo mengi yamejengwa hayana wapangaji lakini sera ya uwekezaji itatusaidia kujua kama inafuatwa. Pia itatusaidia kubaini mapungufu yaliyojiri, maana wajumbe wengi wana wasiwasi kuwa huenda ujenzi wa majengo unalenga kwa wahusika kupata asilimia 10 bila kuangalia mahitaji halisi, kwani majengo mengi yako wazi.”

No comments: