Taarifa Kwa Vyombo Vya Habari Kuhusu Ziara Ya Katibu Mkuu (mawasiliano) Ya Kutembelea Shirika La Posta Tanzania - LEKULE

Breaking

21 Jan 2016

Taarifa Kwa Vyombo Vya Habari Kuhusu Ziara Ya Katibu Mkuu (mawasiliano) Ya Kutembelea Shirika La Posta Tanzania


Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano anayeshughulikia Mawasiliano Prof. Faustin Kamuzora alifanya ziara ya kutembelea Shirika la Posta Tanzania ili kufahamu utendaji kazi na utekelezaji wa majukumu ya Shirika. 
Katika ziara hiyo Prof. Kamuzora aliambatana na Naibu Katibu Mkuu wake Dkt. Maria Sasabo na kufanya mazungumzo na Menejimenti ya Shirika hilo. 
Katika ziara hiyo Prof. Kamuzora alimuagiza Kaimu Posta Masta Kuu wa Shirika la Posta Tanzania Ndugu   Fortunatus Kapinga kuhakikisha kuwa ukusanyaji wa mapato yote ya Shirika la Posta Tanzania (TPC) nchi nzima yanafanyika kwa kutumia njia ya elektroniki ambapo alisema kuwa, “Shirika liboreshe mifumo yake ya kielektroniki ili kupunguza mianya ya wizi na upotevu wa fedha za Shirika na kufanikisha ongezeko la ukusanyaji wa mapato ya Serikali”. 
Prof. Kamuzora aliongeza kuwa Shirika la Posta Tanzania liendane na mabadiliko ili liende kuwahudumia wananchi wa sasa na wa vizazi vijavyo. Shirika ni la kipekee na lina nafasi nzuri ya kutoa huduma kwa wananchi kama ambavyo Shirika kama hili linafanya kazi nzuri  kwenye nchi ya China na Brazil.

Aidha, Prof. Kamuzora aliwaagiza Viongozi wa wasimamizi wa Shirika la Posta Tanzania kutumia Sheria, Kanuni na taratibu za kuwasimamia wafanyakazi na kuwachukulia hatua kali na za kinidhamu watumishi wazembe; wasiotimiza majukumu yao; wasio waaminifu na wabadhirifu.
 Aliongeza kuwa watendaji wafanye kazi na kusimamia Shirika kwa kuwekeana malengo kama inavyojulikana kisheria kwa kutumia Mfumo wa wa Wazi wa Upimaji Utendaji Kazi (OPRAS). 
Alisisitiza kuwa, “Sheria zilizopo zinatosha kumsimamisha mtumishi kazi kwa makosa na hatimaye kumfukuza kazi kwa kuwa watumishi wazembe na wasio waadilifu wanawafanya wananchi wawe na mtazamo hasi na Serikali yao”. 
Prof. Kamuzora alisema kuwa wateja wanahitaji huduma nzuri; ya uhakika na kufikishiwa vifurushi, barua, vipeto na bidhaa nyingine kwa wakati. 
Aliwaagiza viongozi wa Shirika kuangalia uwezekano wa kupunguza gharama za uendeshaji ili kuendesha Shirika kwa tija na faida. Prof. Kamuzora alisema, “Uchumi wa nchi hauwezi kukua wala kwenda popote bila kufanya kazi kwa tija."
Alivitaka vyama vya wafanyakazi visiwatetee watumishi wazembe na vishirikiane na Serikali kufanikisha utekelezaji wa majukumu ya Shirika na watumie mtandao mpana wa Shirika uliopo nchi nzima na kuangalia fursa zilizopo ili kufikisha huduma kwa wateja.

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo anayeshughulikia Mawasiliano ambaye aliambatana na Katibu Mkuu wake Dkt. Maria Sasabo aliagiza kuwa, “Shirika lijipange haraka na kuongeza kasi ya utendaji kazi ya kuwahudumia wateja wake na wananchi ili kuweza kuendana na Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli”. 
Dkt. Maria Sasabo aliongeza kuwa Shirika la Posta lipo nchi nyingi duniani na bado linahitajika hivyo ni muhimu kujipanga kuendana na mahitaji ya sasa ya wateja na Shirika libadilishe utaratibu wa utendaji kazi na kuondoa urasimu ili kuweza kuwahudumia wateja. 
Dkt. Maria Sasabo aliwaagiza viongozi wa Shirika wafanye tathmini na kuangalia namna bora ya kujiendesha ikiwemo kupitia upya muundo na majukumu ya Shirika.

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo anayeshughulikia Mawasiliano Prof. Kamuzora aliuagiza uongozi wa Shirika la Posta Tanzania kuongeza matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kwa kuwa na huduma za ziada za kisasa zinazoendana na mahitaji ya wateja kwa kutumia biashara mtandao kusafirisha na kufanikisha usambazaji wa huduma na bidhaa za wateja kama vile uagizaji wa magari; vitabu na bidhaa nyingine kwa kushirikiana na kampuni kubwa duniani kama vile Alibaba, Amazon na eBay.

Imetolewa na ;

Kitengo cha Mawasiliano Serikalini

No comments: