Majipu 9 Yatumbuliwa Kigoma Kwa Tuhuma Za Ufisadi wa Majengo ya KIGODECO na MIBOS - LEKULE

Breaking

8 Jan 2016

Majipu 9 Yatumbuliwa Kigoma Kwa Tuhuma Za Ufisadi wa Majengo ya KIGODECO na MIBOS


WAKUU wa idara tisa katika Halmashauri ya manispaa ya Kigoma Ujiji mkoani Kigoma, wamesimamishwa kazi kupisha uchunguzi wa tuhuma za ufisadi kwenye matumizi ya fedha na uuzwaji wa majengo ya halmashauri hiyo.

Inaelezwa kuwa kusimamishwa kwa watumishi hao kunafuatia maagizo ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kwa Katibu Tawala wa mkoa huu, John Ndunguru kuunda tume na kufanya uchunguzi kuhusu uuzwaji wa jengo la KIGODECO na MIBOS kutokana na mchakato wa uuzwaji kukiuka sheria ya manunuzi.

Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari hivi karibuni, Ndunguru aliwataja wakuu hao wa Idara kuwa ni pamoja na Ofisa Mipango, Wilfred Mwita, Emanuel Mkwe ambaye ni Mwanasheria, pamoja na Mhandisi wa Ujenzi wa Manispaa hiyo, Boniface William.

Wengine ni Ofisa Biashara, Mussa Igugu, Mkaguzi wa Ndani, Ellymboto Zakharia, Ofisa Misitu wa manispaa hiyo ambaye wakati wa uuzwaji huo alikuwa akikaimu nafasi ya Ofisa Mipango, Leonald Nzilailunde, Ofisa Ugavi, Shida Thadei, Ofisa Mapato, Bawili Mkoko na Fundi Mkuu wa Magari, Omari Rwabibi.

Akizungumzia hatua dhidi ya Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Boniface Nyambele, Katibu Tawala huyo alisema Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) ndiye mwenye jukumu la kumchukulia hatua za kinidhamu na kuzitangaza.

“Watumishi hawa wamesimamishwa kupisha uchunguzi na baada ya uchunguzi kukamilika hatua zaidi zitachukuliwa iwapo itabainika kuhusika kwao, lakini pia Tamisemi italeta timu yao ya uchunguzi kuchunguza suala hilo na imeagizwa kufanya uchunguzi maalumu na CAG katika miradi mbalimbali inayotuhumiwa,” Alisema Ndunguru.

Miongoni mwa mambo yaliyofanya Waziri Mkuu kutoa agizo hilo ni pamoja na mchakato wa uuzwaji wa jengo la KIGODECO ambapo taratibu za kisheria zilikiukwa huku mnunuzi wa jengo hilo ambaye ni benki ya CRDB ikijipa kazi ya kulifanyia uthamini na kutoa bei elekezi ambayo jengo linapaswa kuuzwa.

Aidha, inaelezwa kuwa ilitathminiwa kuwa jengo hilo linapaswa kuuzwa kwa Sh milioni 450, lakini Halmashauri iliamua kuliuza kwa Sh milioni 370.

Ndunguru alisema pia kuwa, kabla ya kununua jengo hilo, CRDB ilipangisha jengo hilo na baadaye Halmashauri ikachukua mkopo kwenye benki hiyo kwa mkataba wa kuifanya benki hiyo itumie jengo hilo kwa miaka mitatu katika mkataba ambao unaeleza kuwa pindi Hamashauri itakapotaka kuvunja mkataba itabidi ilipe tozo kwa benki.

Alisema, Halmashauri hiyo iliamua kuliuza jengo hilo kwa benki ya CRDB na kwamba benki hiyo ilikata deni lake la Sh milioni 50 pamoja na tozo ya Sh milioni 117 kufuatia kuvunjwa kwa mkataba wa ukodishaji ili liuzwe.

Katika tuhuma nyingine, Manispaa ya Kigoma Ujiji inatuhumiwa kuuza jengo la MIBOS kwa Sh milioni 50 bila kulifanyia tathmini huku uthamini ukionesha kuwa bei ya soko kwa sasa kwa jengo hilo ni Sh milioni 72.

Pia, manispaa hiyo inakabiliwa na tuhuma za kubadilisha matumizi ya Sh milioni 809 za miradi ya mifugo, uboreshaji wa miundombinu ya mji wa Kigoma Ujiji na uboreshaji wa miundombinu ya shule za msingi na sekondari katika manispaa hiyo bila kibali.

Hata hivyo, inaelezwa kuwa kikao cha fedha na uongozi kilikataa kuidhinisha fedha hizo kwa ajili ya ujenzi wa maabara za shule za sekondari na badala yake ikaidhinisha matumizi ya Sh milioni 70.


Taarifa hiyo inasema, licha ya kamati ya fedha na uongozi kukataa kuidhinisha matumizi ya fedha hizo, hakukuwa na taarifa iliyotolewa Tamisemi kuhusu jambo hilo na uchunguzi uliofanywa na tume hiyo umebainisha kuwepo kwa shaka katika matumizi ya fedha za kugharimia ujenzi huo wa maabara.

No comments: