Mwanamke kutoka India ‘akatwa mkono’ Saudia - LEKULE

Breaking

11 Oct 2015

Mwanamke kutoka India ‘akatwa mkono’ Saudia

Kasturi Munirathinam
Kasturi Munirathinam amelazwa hospitalini
Wizara ya mashauri ya kigeni ya India imelalamikia serikali ya Saudi Arabia baada ya mwanamke raia wa India kudaiwa kukatwa mkono na mwajiri wake mjini Riyadh.
Mkono wa Kasturi Munirathinam mwenye umri wa miaka 58 alikatwa mkono wa kulia na mwajiri wake alipojaribu kutoroka.
Bi Munirathinam alikuwa akifanya kazi kama mhudumu wa nyumbani. Kwa sasa anaendelea kupata nafuu hospitalini.
Familia yake inadai amekuwa akiteswa na mwajiri wake.
Maafisa nchini Saudia bado hawajazungumzia kisa hicho.
Waziri wa mashauri ya kigeni wa India Sushma Swaraj ameandika kwenye Twitter: "Hili haliwezi likakubalika kamwe. Tumewasilisha malalamiko kwa maafisa Saudia. Ubalozi wetu unawasiliana na mwathiriwa.”
"Kukata mkono wa mwanamke kutoka India – Tumekasirishwa sana na ukatili aliofanyiwa mwanamke huyo wa India nchini Saudi Arabia,” Bi Swaraj aliongeza.
Familia ya Bi Munirathinam katika jiji la kusini mwa India la Chennai imesema mwajiri wa mwanamke huyo alikasirika baada yake kulalamikia mateso aliyokuwa akitendewa nyumbani.
Alikuwa amefanya kazi kwa mwajiri huyo kwa miezi mitatu.
Visa vya watu kutendewa unyama na waajiri wao Mashariki ya Kati vimekuwa vikiripotiwa mara kwa mara, raia wanaotoka Afrika Mashariki wakiwa miongoni mwa waathiriwa.

No comments: