Bawacha: Wanawake Mkipiga Kura Kaeni Mita 200 Mzilinde Zisiibiwe - LEKULE

Breaking

23 Oct 2015

Bawacha: Wanawake Mkipiga Kura Kaeni Mita 200 Mzilinde Zisiibiwe

BARAZA la Wanawake la Chama Cha Demokrasia (Chadema) Taifa, Bawacha, limewataka wanawake nchi nzima kupiga kura na kukaa mita 200 ili kulinda kura zao kwani ni haki yao kisheria.

Kauli hiyo imetolewa juzi na Naibu Katibu Mkuu wa Bawacha Kunti Yusuph wakati wa mkutano na wanawake, uliofanyika katika ofisi za Chadema kanda ya ziwa Victoria jijini Mwqanza.

Mkutano huo uliohudhuliwa na wanawake wengi na kusababisha watu walio wengi kukosa eneo la kukaa kutokana na kunyimwa Uwanja wa Baptist uliopo kona ya Bwiru na halmashauri ya manispaa ya Ilemela, dakika za mwisho licha ya kuwepo taarifa.

Kunti alisema kwa mujibu ya sheria ya uchaguzi ya mwaka 2010, inamruhusu mtu kupiga kura na kukaa mita 200, kutoka kwenye kituo lakini serikali ya CCM inawakataza wananchi kwa kisingizio cha usalama kitendo ambacho ni kinyume na sheria.

“Katika Taifa lolote lile haijawahi kutokea kwamba ukipiga kura uende nyumbani, ndiyo mara ya kwanza kuona kwa Tanzania, hatuwezi kuondoka tutabaki mita 200,” alisema Yusuph.

Kunti ambaye ni mratibu wa mikutano ya kukutana na wanawake ya mke wa Mgombea Urais wa Chadema, Edward Lowassa, Regina Lowassa, alisema kuwa kupitia wanawake wa Mwanza, wanawake nchi nzima wanapaswa kupiga kura na kulinda kura zao.

Alisema endapo wanawake na watanzania kwa ujumla watapiga kura na kuondoka watakuwa wamevunja sheria ya nchi hivyo amewaomba kulinda kura zao kwani ndio maisha yao.

Kwa upande wake Mama Regina Lowassa, alikivaa Chama cha Mapinduzi (CCM) kushindwa kuongea ni nini watawafanyia watanzania na badala yake wamegeuka watukanaji jukwaani.

“Kama CCM wana nia njema na watanzania, kwa nini wasimame jukwaani na kuanza kutukana ninawaomba Wanawake msitishike na watu wa aina hiyo,” alisema Mama Regina.

Pia alisema kuna watu wachache ambao wamekusudia kuharibu uchaguzi kwa lengo la manufaa yao binafsi kitendo ambacho watanzania wanapaswa kuacha kukata tamaa.


Hata hivyo Regina aliwaomba wanawake na watanzania kwa ujumla kukichagua Chadema kuanzia ngazi ya Udiwani, Ubunge na nafasi ya Urais kwa maendeleo ya Taifa.

No comments: