Kikwete: Kuna Uhuru Mkubwa wa Kampeni Kwa Vyama Vyote - LEKULE

Breaking

27 Sept 2015

Kikwete: Kuna Uhuru Mkubwa wa Kampeni Kwa Vyama Vyote


RAIS Jakaya Kikwete amemwambia Kiongozi wa Ujerumani, Kansela Angel Merkel, kuwa upo uhuru mkubwa na usiokuwa kifani kwa vyama vyote ya siasa kufanya kampeni zake kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 25, mwaka huu.

Aidha, Rais Kikwete amemwambia Kansela Merkel kuwa Jopo la Watu Mashuhuri Duniani linalotafuta mapendekezo ya jinsi dunia inavyoweza kujiandaa vizuri zaidi kwa magonjwa ya milipuko, sasa linakaribia kumaliza kazi yake na lipo katika hatua ya kuandaa mapendekezo kuhusu nini dunia ifanye katika siku zijazo.

Rais Kikwete amesema hayo alipokutana na kuzungumza na Kansela Merkel, katika mkutano uliofanyika kwenye Ubalozi wa Ujerumani kwenye Umoja wa Mataifa (UN) mjini New York, ambako viongozi hao walikuwa na mazungumzo ya ana kwa ana.

Viongozi hao wawili wapo New York, Marekani kuhudhuria shughuli za mwaka huu za Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (United Nations General Assembly (UNGA). Katika mazungumzo hayo, Kansela Merkel alitaka kujua kutoka kwa Rais Kikwete kuhusu mwenendo mzima wa kampeni za Uchaguzi Mkuu zinazoendelea nchini na uhuru unaotolewa kwa kila chama kufanya kampeni zake.

“Kama unavyojua Mheshimiwa Kansela tuko katikati ya Kampeni ya Uchaguzi Mkuu. Kampeni zinakwenda vizuri. Tunao wagombea wa urais nadhani kiasi cha wanane hivi na kila chama kinaendesha kampeni zake kwa uhuru mkubwa na usiokuwa na kifani.

Tunataka mchakato ambao utazaa uchaguzi huru na wa haki na hivyo ni muhimu kwa kila chama kuendesha shughuli zake za kampeni kwa uhuru,” alisema Rais Kikwete katika mazungumzo hayo.

Rais pia amemwambia Kansela Merkel kuhusu baadhi ya mambo makubwa ya kampeni yakiwemo yanayohusu masuala ya huduma za kijamii kama vile afya, elimu na mapambano dhidi ya umasikini.

Rais Kikwete pia ametumia mkutano wake na Kansela Merkel kumweleza mama huyo kuhusu kazi ya Jopo la Watu Mashuhuri Duniani kuhusu Matatizo ya Afya, akisisitiza kuwa baada ya hatua ya kuwasikiliza watu mbali mbali, sasa jopo limeanza kuandaa maoni yake na mapendekezo.


Jopo hilo lililoteuliwa Aprili mwaka huu na Katibu Mkuu wa UN, Ban Ki-moon baada ya kutokea majonzi makubwa yaliyosababishwa na ugonjwa wa ebola katika nchi za Guinea, Liberia na Sierra Leone, linatarajiwa kukabidhi ripoti yake kwa Ban Ki-moon Desemba mwaka huu.