JWTZ Yawataka Watu Waliozusha Kuwa Mkuu wa Majeshi, Jenerali Davis Mwamunyange Ni Mgonjwa Waombe Radhi Haraka - LEKULE

Breaking

27 Sept 2015

JWTZ Yawataka Watu Waliozusha Kuwa Mkuu wa Majeshi, Jenerali Davis Mwamunyange Ni Mgonjwa Waombe Radhi Haraka


WIZARA ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, imewataka watu waliosambaza uvumi katika mitandao ya kijamii kuwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi nchini, Jenerali Davis Mwamunyange, kuwa amelazwa nje ya nchi kwa ugonjwa, kuomba radhi mapema la sivyo watachukuliwa hatua.

Taarifa iliyotolewa jana na msemaji wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Luteni Kanali Juma Sipe, imeweka wazi kuwa Jeshi na Wizara kwa kushirikiana na mamlaka husika, wanachunguza watu hao na kuwataka waombe radhi mapema kabla ya hatua hizo.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Jenerali Mwamunyange ni mzima wa afya na aliondoka nchini Jumanne iliyopita Septemba 22, 2015, saa 10.45 jioni kwa ndege ya Shirika la Ndege la Emirates kwenda Rome, Italia kwa ziara ya kikazi kwa mwaliko wa Mkuu wa Majeshi wa nchi hiyo, Jenerali Claudio Graziano.

“Tunapenda kuwahakikishia wananchi kuwa Jenerali Mwamunyange pamoja na ujumbe wake wanaendelea na ziara hiyo kama ilivyopangwa na amesikitishwa na uvumi huo,” alisema Sipe.

Sipe alisema uvumi huo ni matumizi mabaya ya uhuru wa habari na kuupotosha umma na umeleta usumbufu kwa familia ya Jenerali Mwamunyange, Jeshi na Taifa kwa ujumla. 
 
Alisisitiza kuwa watu walisambaza uzushi huo kwamba Jenerali Mwamunyange amelazwa katika Hospitali ya Aga Khan iliyopo Nairobi, Kenya, huku wengine wakidai kuwa yuko nchini India kwa matibabu, kumuomba radhi kwa kutambua kuteleza kwao.

“Taarifa hizo ni uongo wenye kila dalili ya kutengenezwa kwa lengo la kuwatia hofu Watanzania juu ya usalama wa kiongozi huyu wa juu wa majeshi yetu, Mkuu huyo wa Majeshi ya Ulinzi, ni mzima wa afya na hayupo nchini Kenya wala sio India kama ilivyoenezwa kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari,” alisema Sipe.


Sipe alionya kwamba kuacha kuomba radhi, itatafsirika kuwa ni kukiri kueneza uzushi huo kwa makusudi na kwa dhamira fulani na hivyo kushawishi hatua zaidi kuchukuliwa. Alisema wizara hiyo imesikitishwa na tabia hiyo ya uzushi inayopingana na weledi na kanuni za uandishi wa habari.
 Jenerali Mwamunyange akikagua gwaride lililoandaliwa kwa heshima yake na mwenyeji wake Rome, nchini Italia.
 Jenerali Mwamunyange akikagua gwaride lililoandaliwa kwa heshima yake na mwenyeji wake Rome, nchini Italia.
Jenerali Mwamunyange akiteta jambo na mwenyeji wake Rome, nchini Italia.