Ajali ya Basi Yaua Watu Watano.....Chanzo cha Ajali ni Dereva Kusinzia - LEKULE

Breaking

16 Sept 2015

Ajali ya Basi Yaua Watu Watano.....Chanzo cha Ajali ni Dereva Kusinzia


Watu watano wamekufa na wengine 39 kujeruhiwa vibaya baada ya basi walilokuwa wakisafiria la kampuni ya Metro kuacha njia na kupinduka katika eneo la Manga, mpakani mwa mikoa ya Tanga na Pwani, chanzo kikidaiwa dereva alikuwa akisinzia.

Waliokufa katika ajali hiyo iliyotokea jana ni Joseph John (45) na Joseph Shayo (41), wakazi wa Moshi, mkoani Kilimanjaro na Zakaria Kintupa, mkazi wa Lutindi na mwanawe ambaye jina lake halikufahamika mara moja.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Zuberi Mwombeji, amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kwamba  miili ya marehemu na majeruhi wa ajali hiyo wamepelekwa katika Kituo cha Afya cha Mkata, wilaya ya Handeni, mkoani Tanga.

Kwa mujibu wa Kamanda Mwombeji, ajali hiyo  ilitokea saa 5.00 asubuhi wakati basi hilo likitokea Dar es Salaam kuelekea Rombo, mkoani Kilimanjaro.

Alisema basi hilo lilipinduka baada ya dereva kushindwa kumudu kona kali na hivyo kuacha njia na kuingia kwenye korongo.

Hata hivyo, baadhi ya abiria waliokuwa wakisafiri na basi hilo walidai ajali hiyo ilitokea kutokana na dereva kuendesha huku akisinzia.


Kamanda Mwombeji alisema dereva wa basi hilo ambaye jina lake halikufahamika alitoroka baada ya ajali hiyo kutokea na kwamba polisi wanaendelea kumsaka, huku mmiliki wa basi akihojiwa na kwamba uchunguzi wa ajali hiyo ili kujua chanzo chake halisi unaendelea.

No comments: