Kesi ya Askari Polisi Kuiba silaha, Risasi Yaahirishwa - LEKULE

Breaking

22 Jun 2015

Kesi ya Askari Polisi Kuiba silaha, Risasi Yaahirishwa

KESI ya wizi wa silaha aina ya SMG na risasi zake 42 inayomkabili aliyekuwa Konstebo wa Polisi, GX 7274, Hamad Taimu Shilingi (25) katika Mahakama ya Wilaya ya Sumbawanga mkoani Rukwa imeahirishwa hadi Julai Mosi mwaka huu.
 
Hakimu wa Mahakama hiyo, Enock Matembele aliamuru mshtakiwa arudishwe rumande hadi Julai Mosi mwaka huu ambapo mahakama hiyo itaamua iwapo mshtakiwa huyo apewe dhamana au la.
 
Mshtakiwa huyo alifikishwa mara ya kwanza Mei 26 mwaka huu ambapo upande wa mashtaka ulipinga asipatiwe dhamana kwa kuwa bado upelelezi wa shauri hilo unaendelea ambapo upande wa utetezi uliwasilisha mahakamani hapo kiapo cha pingamizi .
 
“Uamuzi kuhusu mshtakiwa apewe dhamana au la utatolewa na Mahakama hii hapo Julai Mosi mwaka huu hivyo mshtakiwa atarudi rumande hadi tarehe hiyo,“ alieleza Hakimu Matembele mahakamani hapo.
 
Kwa mujibu wa hati za mashtaka mahakamani hapo mshtakiwa alitenda kosa hilo Aprili 4 , mwaka huu katika Kituo cha Polisi mjini Namanyere wilayani Nkasi ambapo anadaiwa kuiba silaha aina ya SMG yenye nambari 21084.
 
Ilidaiwa mahakamani hapo kati ya Aprili 04 na Mei 19 mwaka huu mshtakiwa huyo aliiba risasi 42 za SMG kutoka katika kituo kikuu hicho cha Polisi mjini Namanyere wilayani Nkasi.
 
Kabla ya kufikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza, Mei 26 mwaka huu mbele ya Hakimu Matembele, mshtakiwa huyo Mei 22 alifikishwa na kuhukumiwa katika Mahakama ya Kijeshi.

No comments: