HILDA: Wakili wa Serikali anayechukizwa na wanaume wanaonyanyasa wake zao - LEKULE

Breaking

18 May 2015

HILDA: Wakili wa Serikali anayechukizwa na wanaume wanaonyanyasa wake zao


Dar es Salaam. 
“Ni vigumu kumudu kazi na familia kwa wakati wote kutokana na ukweli kwamba mwanamke anakabiliana na majukumu mengi ikiwamo ya kazini, kuhudumia familia na wakati huohuo kuangalia mume, lakini hatuna budi kukabiliana na changamoto hizi ili kuwa na familia bora.”
Ndivyo anavyoanza kusema Hilda, Wakili wa Serikali katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Idara ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP).

Mwenyewe anasema kilichomwezesha kufika hapo ni juhudi zake za kupenda kujiendeleza na kusoma hasa ukizingatia fani hiyo aliipenda tangu akiwa mdogo.

Hilda ambaye ni mama wa watoto wawili, anasema dhamira ya kuwa mwanasheria ilichagizwa na tamthilia aliyowahi kuiangalia ya ‘Inspector Dereck’na ambaye katika tamthilia hiyo alionekana akizungukazunguka mahakamani akiwa amevaa suti yake nyeusi yenye kumpendeza.
“Ukweli ni kwamba nilikua nikivutiwa sana na mavazi ya wanasheria wakiwa mahakamani na hii ndiyo ilinifanya nisome kwa bidii kwa kuamini kuwa ipo siku ndoto yangu itatimia na kufikia malengo yangu,” anasema Hilda (34).

Kwa mujibu wa Hilda, alitamani siku moja kuwa mwanasheria ili kuwahudumia watu wenye matatizo mbalimbali ikiwamo unyayasaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto, migogoro ya kifamilia na ardhi, kutoa haki pamoja na kutoa msaada wa kisheria kwa watu wanaohitaji.
Hilda ambaye kwa sasa ni mwendesha mashtaka wa Serikali katika Wilaya ya Ilala, anasema safari yake hadi kufikia hapo haikuwa rahisi kwani alipitia changamoto mbalimbali lakini hakukata tamaa kufikia malengo yake.

Muda wa kazi na familia:

“Huku mtoto anahitaji uangalie kazi yake aliyofanya shuleni, huku mume anakuhitaji umbembeleze, wakati huo huo unawaza kesi mahakamani, hii ni changamoto inayopaswa kukubaliana nayo cha msingi ni kuhakikisha kila kitu kinafanywa kwa wakati wake.”
Anasema kinachotakiwa kwa wanawake ni kupangilia muda wa kazi na muda wa majukumu ya nyumbani na hali hiyo itasaidia kuwa na familia yenye furaha na siyo kila wakati kumuachia mfanyakazi wa nyumbani kwa kisingizio cha kazi.

Hata hivyo, Hilda anasemea hapendi kuona wanaume wananyanyasa wake zao huku akiwataka wanawake wajishughulishe katika biashara za ujasilimali ili kujenga familia bora.
Anasema hali hiyo inasababisha wanawake wengi kukata tamaa hivyo hutumia muda wake wa ziada kutoa msaada wa kisheria pamoja na kuwapa matumaini wale ambao wanamigogoro.

“Nachukia kuona watoto wakiteseka mitaani na kuvunjika kwa familia kwa hali hii huwaathiri zaidi watoto na kuwapotezea ndoto zao za baadaye, hivyo nawashauri wa wanawake wenzangu kumshirikisha Mungu ili kuzinususru.” anasema Hilda na kuongeza kuwa kesi nyingi za wanandoa huwaathiri sana watoto wao. Mwanasheria huyo ambaye shahada yake ya kwanza ya sheria aliyoichukua mwaka 2001 katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Anapokuwa nyumbani anafanya nini?

Hilda anasema anapenda kutengeneza bustani ya maua kwani inafanya nyumba iwe na mwonekano wa kuvutia. Anasema sambamba na kujihusha na masuala ya bustani akiwa nyumbani pia ni hupenda kupika, kusoma vitabu, kuangalia kazi za shule za watoto wake na kuangalia luninga ili kujua vitu vinavyojiri ulimwenguni.

No comments: