Mhe. Jenista Aagiza Kamati Za Menejimenti Ya Maafa Nchini Kuwatoa Wanaoishi Kwenye Maeneo Hatarishi Mara Moja ......Vinginevyo Kamati Itawajibishwa - LEKULE

Breaking

23 Dec 2015

Mhe. Jenista Aagiza Kamati Za Menejimenti Ya Maafa Nchini Kuwatoa Wanaoishi Kwenye Maeneo Hatarishi Mara Moja ......Vinginevyo Kamati Itawajibishwa


TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
UTEKELEZAJI WA AGIZO LA MENEJIMENTI YA MAAFA KWA KAMATI ZA MAAFA NGAZI ZA MIKOA, WILAYA, KATA NA VIJIJI

Kufuatia taarifa ya tahadhari ya uwezekano wa kuwepo kwa mvua za El-Nino iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Mwezi Agosti 2015, Ofisi ya Waziri Mkuu ilitoa agizo kwa Mikoa yote nchini kuchukua hatua za kujiandaa na kukabiliana na maafa yanayoweza kutokea kutokana na mvua hizo. 
 
Kamati za Maafa za Mikoa, Wilaya, Kata na Vijiji ambazo ndizo zenye jukumu kubwa la kusimamia masuala haya, hazijatekeleza agizo hilo kwa kuainisha hatua zilizochukuliwa katika Kuzuia/Kupunguza, Kujiandaa, Kukabili na Kurejesha hali baada ya maafa kutokea. Hivyo;
 
“Naagiza wenyeviti wa kamati za maafa katika ngazi husika kwa kushirikiana na taasisi na idara za serikali zinazohusika waorodheshe watu wote wanaoishi katika maeneo hatarishi na kuwapa barua za kuwataka kuhama mara moja katika maeneo hatarishi ili kuepuka athari za maafa. 
 
"Taarifa za utekelezaji wa agizo hili ziwasilishwe katika Ofisi ya Waziri Mkuu haraka sana kadri iwezekanavyo” amesema Mhe. Mhagama. 
 
Ili kutekeleza agizo hili ninaziagiza Kamati za maafa za Mikoa, Wilaya, Kata na Vijiji ziwajibike kutekeleza mambo yafuatayo;
 
I. Kamati zote ambazo hazijatekeleza maagizo yaliyotolewa na viongozi katika kushughulikia maafa zitoe maelezo ya kwanini hazijatekeleza maagizo hayo kwa mamlaka husika.
 
II.Endapo kutatokea maafa mahali popote katika nchi yetu kwa sasa, kamati za maafa zitawajibika kuelezea sababu za kutokea kwa maafa hayo ni nini katika maeneo yao na kuainisha hatua zilizochukuliwa na kamati hizo za kukabili hali hiyo iliyojitokeza. Lakini taarifa hizo pamoja na kuwasilishwa kwenye mamlaka husika pia ziwasilishwe kwenye vyombo vya habari. 
 
III.Kamati zote za maafa katika ngazi zote, zitoe maelezo na mipango waliyonayo juu ya kupambana na mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu janga ambalo linasababisha maafa katika nchi yetu.
 
IV. Kamati zote za maafa katika ngazi zote, zishirikishe wadau wa maafa (Wananchi, Taasisi na Sekta binafsi) katika mipango yao yote ya kukabili maafa ya menejimenti ya maafa.
 
V.Kamati zote za maafa ziendelee kuratibu na kutoa taarifa juu ya misaada yote ya maafa inayotolewa na Serikali pamoja na wadau katika kusaidia waathirika wa maafa pale yanapotokea.
 
VI.Kamati hizo za maafa katika ngazi zote zinatakiwa, kuchukua /kumchukulia hatua mtendaji na mhusika mwingine yeyote ambaye hatatimiza wajibu wake na kutotekeleza maagizo yanayotolewa na viongozi nchini katika kukabili maafa mahali popote.
 
“Serikali inawaomba wadau wote wa maafa ushirikiano wa hali ya juu katika jambo hili muhimu katika nchi yetu ili kuweza kuokoa watanzania wengi ambao wanaweza kukumbwa na maafa kwa namna moja ana nyingine”, amesisitiza Mhagama 
 
Aidha, Sheria Na. 7 ya Mwaka 2015 ya Menejimenti ya Maafa inamtaka kila mdau kutekeleza wajibu wake katika suala zima la menejimenti ya maafa ikiwa pamoja na Kuzuia, Kujiandaa, Kukabili na Kurejesha hali baada ya maafa kutokea. 
 
“Napenda kuchukua fursa hii kuzikumbusha Kamati za maafa katika ngazi za Mikoa, Wilaya,Kata na Vijiji kuhakikisha kuwa zinatimiza wajibu wao katika suala zima la kushughulikia maafa kwa mujibu wa sheria” amesema Mhe. Mhagama. 
 
Hivi sasa sehemu mbalimbali za nchi yetu zimekuwa zikipata mvua nyingi ambazo zimesababisha maafa na baadhi ya sehemu zinakabiliwa na ukame. 
 
Taarifa nyingi zilizopokelewa zinaonesha baadhi ya maeneo ya nchi yetu yamekuwa yakipata mvua nyingi ambazo zimesababisha maafa bila Kamati za Maafa za Mikoa, Wilaya,Kata na Vijiji kuainisha hatua zilizochukuliwa katika Kuzuia/Kupunguza, Kujiandaa, Kukabili na Kurejesha hali baada ya maafa kutokea.
 
Iwapo juhudi za ngazi zote pamoja na Mkoa zitashindwa kukabili maafa yanayotokea katika ngazi za Wilaya, Kata na Vijiji, taarifa na maombi zitumwe katika ngazi ya Taifa kwa kuzingatia maelekezo/mwongozo wa uombaji wa misaada na utoaji wa taarifa za maafa uliotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu.
Imetolewa na

JENISTA J. MHAGAMA (MB)
WAZIRI WA NCHI OFISI YA WAZIRI MKUU
SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WATU WENYE ULEMAVU

22 DESEMBA 2015

No comments: