MKUU WA MKOA WA MOROGORO AWATIA NDANI WACHINA WAWILI KWA KUKAIDI AGIZO LA SERIKALI - LEKULE

Breaking

15 Apr 2016

MKUU WA MKOA WA MOROGORO AWATIA NDANI WACHINA WAWILI KWA KUKAIDI AGIZO LA SERIKALI


Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dk. Kebwe Steven Kebwe, (katikati) pamoja na ujumbe wake wakifanya ukaguzi wa kushitukiza katika mgodi wa Kiwanda cha Tanzania Zhong Fa Construction Material Group Co Ltd , katika mgodi wa Kiwanda hicho uliopo eneo la Kitongoji cha Mazizi, Kijiji cha Maseyu, Kata ya Gwata, Tarafa ya Mikese, wilaya ya Morogoro, kiwanda hicho kinamilikiwa na wachina, uzalishaji wake ulizuiwa na Serikali kuu tangu mwaka 2010 hadi watakapokamilisha taratibu zote za kisheria zikiwemo na za kimazingira.
Mfanyakazi raia wa China, Wang Jun (33) ambaye ni mtunza stoo katika mgodi wa kutengeneza marumaru wa Kiwanda cha Tanzania Zhong Fa Construction Material Group Co Ltd ,kinachomilikiwa na Wachina akiwa chini ya ulinzi wa Polisi kufuatia ukaguzi wa ghafla wa mkuu wa mkoa wa Morogoro Dk Kebwe Steven Kebwe, Aprili 13,2016 akifuatana na ujumbe wa serikali ya mkoa na wilaya ya Morogoro katika mgodi wa Kiwanda hicho uliopo Kitongoji cha Mazizi, Kijiji cha Maseyu, Kata ya Gwata, Tarafa ya Mikese , ambapo walikutwa wakiendelea na uzalishaji licha kuzuiwa na Serikali kuu mwaka 2010 hadi watakapokuwa wamekamilisha taratibu zote za kisheria zikiwemo na za kimazingira.

Na John Nditi, Morogoro

RAIA  wawili wa China wametiwa nguvuni mkoani Morogoro kutokana na kuendelea kusimamia shughuli za uzalishaji wa marumaru katika mgodi wa mawe wa Kiwanda cha Zhong Fa Construction Material Group Co Ltd ,kinachomilikiwa na Wachina licha ya kuzuiwa na Serikali kuu tangu mwaka 2010.

Mbali na kuendelea na uzalishaji katika kipindi chote hicho, kampuni hiyo imekuwa ikifanya udangayifu  kuwa marumaru  zinazouzwa katika maduka yake zinaingizwa kutoka  nchini China , wakati bidhaa hiyo ikitengenezwa  kutoka Morogoro.

Mkuu wa mkoa wa Morogoro, Dk Kebwe Steven Kebwe, aliamuru kukamatwa kwa raia hao  baada ya kufanya  ukaguzi wa kushitukiza   Aprili 13, 2016  akiwa na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa  pamoja na viongozi wa halmashauri ya wilaya ya Morogoro.

 Kampuni  hiyo ilizuiwa kuendelea na uzalishaji wa marumaru katika mgodi  uliopo  katika Kitongoji cha Mazizi, Kijiji cha Maseyu, Kata ya Gwata, Tarafa ya Mikese tangu Novemba 30, mwaka  2010 , lakini imeendelea  na uzalishaji  kwa kipindi chote hicho bila kuwa na vibali  wala taratibu zote za kisheria zikiwemo za   hifadhi ya  kimazingira.

Hatua ya Mkuu kufanya  ziara hiyo ni kwenda kujiridhisha kutokana na taarifa ya  uongozi wa halmashauri ya wilaya ya Morogoro iliyowasilisha  vielelezo mbalimbali juu ya  kampuni hiyo kushindwa kulipa tozo la  kiasi cha Sh milioni sita kwa hesabu za wakati huo kabla ya kuzuiwa na Serikali.

Dk Kebwe alisema, licha ya  kuzuiwa  na  Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo ,wakati wa Serikali ya awamu ya nne  kabla ya  mabadiriko ya wizara hiyo  baada ya Waziri kutembelea mgodi huo na kukuta wakiendesha uzalishaji bila kuwa na leseni na vibari kutoka katika mamkala mbalimbali ikiwemo  ya wizara hiyo .

“ Tangu wakati wa Waziri Profesa Muhongo awamu ya kwanza walipozuiwa kuendea na uchimbaji hadi watakapo kamilisha utaratibu wa kisheria zikiwemo na za hifadhi ya kimazingira,  wameendelea kuzalisha katika mgodi bubu ...wamechimba eneo na kurivuruga kimazingira “ alisema Mkuu wa Mkoa Dk Kebwe.

 Dk Kebwe alisema , uzalishaji wa marumaru katika mgodi huo umekuwa ikiendelea kwa njia zisizo halali ambapo bidhaa hiyo inatengezwa eneo hilo na kusafirishwa katika maduka ya Kampuni hiyo yaliyopo Jijini Arusha na Dar es Salaam kwa ajili ya kuuzwa ndani na nje ya nchi.

“ Ufuatiliaji umekuwa ukifanyika mara kwa mara eneo la mgodi na uzalishaji umekuwa ukifanyika kama tulivyowakuta  hapa na marumaru hizi zikifikishwa katika maduka hayo zinajazwa kwenye makadha yaliyoandikwa kwa lugha ya kishina ya kampuni hii na kuonesha zimeingizwa kutoka China na kuuzwa ka bei ghali “ alisema Dk Kebwe.

“ Tumenunua marumaru zilizo kwenye maduka haya na kubaini hazitoki China bali ni Morogoro kwenye mgodi unaozalisha bidhaa hizi na kuwekwa nembo ya Kichina kwa jina hilo la kampuni ...huu ni wizi na kuikosesha serikali  na halmashauri mapato  yake” alisisitiza Mkuu wa mkoa , Dk Kebwe.

Mkuu wa mkoa , Dk Kebwe alisema , tangu mwaka 2010 walipozuiwa na Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini, uzalishaji umeendelea kukua katika mgodi huo  ambapo  marumaru hizo kwa sasa zinasafirishwa kuuzwa katika nchi jirani za Afrika Mashariki na Kati zikiwa na lebo ya kutoka nchini China.

“ Kutokana na udanganyifu na wizi unaofanyika ndiyo maana kiwanda hiki hakijafungua Duka hapa Morogoro isipokuwa ni Dar es Salaam na Arusha ili watanzania wajue ni bidhaa kutoka China ,  na bei ya chini ya marumaru moja ndogo ni Sh 280,000 , jambo hilo lazima tulikomeshwe “ alisema Dk Kebwe.

Pia  Dk Kebwe aliitaka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Morogoro kuanza mara moja kufanya tathimini ya mauzo ya marumaru  zinazotokana na uzalishaji wa mgodi huo  ili kupata  mauzo halisi ya  Kampuni ili kuiwezesha halmashauri kupata  malipo ya halali .

Kutokana na kukaidi agizo la Serikali , mkuu wa mkoa Dk Kebwe aliamuru kukamatwa kwa wafanyakazi wawili wa China wa  Kiwanda cha  Zhong Fa Construction Material Group Co Ltd  na msimamizi wa kitanzania  kwa lengo la kuisaidia   serikali ya mkoa katika uchunguzi wake  juu ya  kiwanda hicho.

Wachina waliokamatwa  na Polisi  eneo la mgodi  ni Mtunza stoo Wang Jun (33) na mwezake Shiqing Liang (36)  ,wakati  mtanzania ni  Hilary Paulo.

Naye Ofisa Madini Mkazi wa  Mkoa wa Morogoro, Bertha Luzabiko, alimwezeza mkuu wa mkoa kuwa  licha ya kuhamia  mkoa huo mnamo Novemba mwaka 2014 , kazi yake ya kwanza ilikuwa ni kushughulikia maombi ya Kampuni hiyo , lakini iligundulika kuwa  eneo  hilo tayari lina  leseni ya  mwekezaji mwingine  na si  rahisi kutolewa nyingine.

Luzabiko alisema  aliwaadikia barua  wenye  mgodi huo ya  kuwasimamisha  kuendelea na kutokana na eneo hilo lina leseni ya mtu mwingine  wa  uchimbaji wa dhahabu.

Hivyo alisema  baada ya kuwandikia barua ya kusitisha shughuli zao , aliamua kufanya mara tatu kwa nyakati tofauti alikuta shughuli uchimbaji na  utengenezaji wa marumaru ukiendelea , ndipo alipoamua kuripoti Polisi ili watu hao wakamatwe na kufunguliwa kesi mahakamani zoezi ambalo lilifanyika.

Lizabiko alisema,  licha ya kukamatwa kwao, bado waliendelea   na uzalaishaji ambapo pia aliamua kulifikisha   suala hilo  kwa Kamishina wa Madini Kanda ya Mashariki aliyemtaja kwa jina la Hamis Komba  ili kuchukua  hatua za kisheria na kiutawala.

Naye Meneja wa Mamlaka ya  Mapato Tanzania (TRA), mkoa wa Morogoro  Philip Kimune , aliyefuatana na Mkuu wa mkoa eneo la mgodi huo alisema taarifa zilizipo kwenye  Mamkala ya Mapato  zinaonesha kuwa  , kampuni hiyo inatumia  jina la Tanzania Zhong Fa Construction Material Group Co Ltd.

Alisema ,kwa  kipindi cha kuanzia mwaka 2011 hadi Machi 2016  kiwanda hicho kilionesha  kuwa mauzo  ya kiasi cha Sh bilioni 30.9 yaliyolipiwa  Vat ya Sh bilioni 5.5.

Mbali na hayo alisema , mauzo hayo hayakuonesha  iwapo   yalitokana na bidhaa ya marumaru  ama yalijumuishwa  na bidhaa nyinginezo  zinazozalishwa na  kampuni hiyo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo, Yona Maki alisema , kuchelewa kwa mchakato wa kukusanya ushuru katika kiwanda cha kuchoronga mawe cha wachina  kinaikoseha mapato halmashauri  kiasi cha zaidi ya Sh milioni 90 kwa kipindi cha miaka  sita  kuanzia mwaka 2010.
Sehemu ya Muonekano wa Kiwanda hicho.
Mfanyakazi wa Mgodi huo, Hilary Paulo (kulia) akimpatia maelezo Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Dk. Kebwe Steven Kebwe. 




No comments: