Kiwanda cha Mount Meru Millers Chafungwa na Kutozwa Faini ya Milioni 12 Kwa Uharibifu wa Mazingira - LEKULE

Breaking

3 Apr 2016

Kiwanda cha Mount Meru Millers Chafungwa na Kutozwa Faini ya Milioni 12 Kwa Uharibifu wa Mazingira


Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), limekifunga kiwanda cha Mount Meru Millers Ltd kilichopo wilayani Bunda, mkoani Mara na kukipiga faini ya Sh12 milioni kwa uharibifu wa mazingira kinyume cha Sheria ya Kulinda na Kuhifadhi Mazingira.

Hatua hiyo ya NEMC imekuja baada ya malalamiko  ya muda mrefu  kuhusu kiwanda hicho kutiririsha maji yenye kemikali zenye sumu katika makazi ya watu, vyanzo vya maji na kwenye mashamba ya mpunga.

Mratibu wa NEMC Kanda ya Ziwa, Anna Mdamo alisema uchunguzi uliofanywa na baraza hilo Machi 22, mwaka huu, ulibaini kuwa kiwanda hicho kinaendesha shughuli zake kinyume cha Sheria ya Mazingira ikiwa ni pamoja na kutokutumia mtambo wa kutibu maji kabla ya kuyaachia kuingia mitaani.

Mmoja wa viongozi wa kiwanda hicho aliyezungumza kwa sharti la kutotajwa jina alikiri kupokea barua ya kukifunga toka juzi.

Kwa mujibu wa NEMC, kiwanda hicho kinatakiwa kulipa faini ndani ya siku 14, vinginevyo hatua zaidi zitafuata ikiwamo kufikishwa mahakamani.


Mkuu wa Idara ya Mazingira ya Halmashauri ya Mji wa Bunda, Majura Masumbuko aliishukuru NEMC kwa kuchukua hatua dhidi ya kiwanda hicho kilichosababisha mgogoro kati ya mamlaka za Serikali wilayani Bunda. 

No comments: