Wito wa Kufanya Usafi Kila Jumamosi ya Mwisho wa Mwezi - LEKULE

Breaking

23 Mar 2016

Wito wa Kufanya Usafi Kila Jumamosi ya Mwisho wa Mwezi

Watanzania Wenzangu mtakumbuka kwamba tulikubaliana tuwe tunafanya usafi wa mazingira yetu nchi nzima kila jumamosi ya mwisho wa mwezi ili kuitikia wito wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliouanzisha tarehe 09 Desemba 2015.

Nachukua nafasi hii kuwasihi Watanzania wote kushiriki kikamilifu kufanya Usafi wa Mazingira kwenye Makazi yetu, Maeneo yetu ya Biashara, maeneo ya Taasisi za Umma na maeneo yenye mikusanyiko ya watu mbalimbali kama masokoni na minadani.

Mbali ya kwamba kufanya usafi kuna fanya mazingira yetu yapendeze na hivyo kuondoa magonjwa yanayo sababishwa na uchafu lakini pia zoezi la kufanya usafi kwa pamoja lina jenga Umoja na Mshikamano wa kitaifa, linaondoa matabaka ndani ya jamii yetu.

Natoa wito kwa kila Mtanzania Kujitokeza kufanya usafi bila kujali uwezo wa mtu,hadhi yake,cheo chake, au nafasi yake katika jamii. Viongozi wa makundi yote katika jamii tuwe mfano katika jambo hili jema.

Nichukue fursa hii kusisitiza tuendelee kujitokeza kufanya Usafi ili Utamaduni huu ujengeke kwa Kizazi cha sasa na kizazi kijacho.

Watanzania wote wa Mijini na Vijijini tujenge desturi ya kuweka mazingira yetu katika hali ya usafi wakati wote na katika jambo hili kila mmoja wetu awe mlinzi wa kukemea watu wenye tabia za kutupa taka hovyo ili maeneo yetu yawe katika hali ya usafi na yakuvutia wakati wote.

Usafi kwenye nyumba na mazingira yako,Usafi kwenye sehemu ya Shughuli zako na mazingira yake ndio usafi wa Taifa. Tujitokeze,Tuungane tukafanye Usafi kila Jumamosi ya Mwisho wa Mwezi kuanzia saa 12 Asubuhi
Asanteni.

Imetolewa na:
George B. Simbachawene (Mb)
WAZIRI WA NCHI
OFISI YA RAIS - TAMISEMI

No comments: