Viongozi wa Dini Wazidi Kutofautiana Kuhusu Sakata La Zanzibar.......Sheikh Ponda Issa Ponda Apinga Uchaguzi Kurudiwa Zanzibar - LEKULE

Breaking

4 Feb 2016

Viongozi wa Dini Wazidi Kutofautiana Kuhusu Sakata La Zanzibar.......Sheikh Ponda Issa Ponda Apinga Uchaguzi Kurudiwa Zanzibar



Mgogoro kuhusu kurudiwa kwa uchaguzi viswani Zanzibar unazidi kupasua nchi, sasa viongozi wa Dini ya Kiislam wametofautiana.

Ikiwa ni siku moja baada ya Alhad Mussa Salum ambaye ni Sheikh Mkuu wa Dar es Salaam kuunga mkono Tume ya Uchaguzi wa Zanzibar (ZEC) kutangaza tarehe ya uchaguzi visiwani humo, Jumuiya ya Taasisi za Kiislam Tanzania imepinga.

Sheikh Ponda Issa Ponda, Katibu wa Jumuiya ya Taasisi za Kiislamu nchini katika mkutano wake na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam amesema, kuruhusu kurudiwa kwa uchaguzi visiwani humo ni kupandikiza mbegu za chuki kwa wananchi.

Sheikh Ponda amesema kuwa uchaguzi uliofanyika Oktoba mwaka jana haukuwa na mashaka kwa kuwa, waangalizi wa nje pia walithibitisha hilo.

“Ripoti za waangalizi wa ndani na nje zilithibitisha kuwa uchaguzi haukuwa na dosari. Kuna sababu gani ya kurudia uchaguzi,” amehoji Sheikh Ponda.

Wakati Sheikh Ponda akihoji sababu za ZEC kutaka kurudiwa kwa uchaguzi huo, Sheikh Alhad aliipongeza tume hiyo na kuongeza“tunaiomba ZEC kusimamia kazi hii kwa haki, uadilifu na umakini mkubwa…”

Sheikh Alhad jana alisema kuwa Baraza la Waislam Tanzania (BAKWATA) linaunga mkono uamuzi wa ZEC kurudia uamuzi huku akikitaka Chama cha Wananchi (CUF) ambacho kimesusia uchaguzi huo, kushiriki.

CUF kwenye mkutano wake wa Baraza Kuu uliofanyika tarehe 27 na 28 Januari mwaka huu kilieleza kususia uchaguzi huo uliopangwa kufanyika tarehe 20 Machi mwaka huu na kudai kuwa, hakuna sababu yoyote kwa chama hicho kushiriki. ZEC ilifuta uchaguzi huo tarehe 28 Oktoba mwaka jana.

Hata hivyo, Sheikh Ponda amesema kuwa, ZEC haikuwa na sababu ya kufuta uchaguzi  kwa kuwa, baada ya tume hiyo kutangaza matokeo, haina mamlaka ya kufuta.

Pamoja na kupinga kurudiwa kwa uchaguzi, Sheikh Ponda Sheikh Alhad amepata wapi kauli ya Kiongozi wa Jumuiya za Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (Jumiki), Sheikh Farid Hadi Ahmed kuwa anaunga mkutano marudio ya uchaguzi Zanzibar.

Sheikh Alhad kwenye mkutano wake jana alisema “Hata kiongozi wa Uamsho, Sheikh Farid Ahmad pia anaunga mkono suala la kufanyika uchaguzi wa marudio kwa mujibu wa barua yake aliyonitumia mimi .”

Sheikh Ponda ameeleza kwamba, Sheikh Farid hawezi kutoa kauli hiyo na kwamba kama Sheikh Alhad anayo barua hiyo, aitoe hadharani.

“Sio jambo rahisi kuamini kwamba Sheikh Farid anaweza kutoa kauli hiyo, sio jambo rahisi kabisa na kama ni kweli basi atoe ushahidi wake,”ameeleza Sheikh Ponda.

Pia Sheikh Ponda ameonesha kushangazwa na ZEC kuhalalisha matokeo ya Rais wa Muungano wa Tanzania sambamba na Wabunge wa Bunge la Muungano.

Shekh Ponda amesema kuwa uchaguzi wa Zanzibar na matokeo yake bado ni halali “Sisi kama Tasisi ya Waislamu tunapinga kurudiwa kwa uchaguzi wa Zanzibar.”

Amesema kuwa, taasisi hiyo imeunga mkono hatua za mwanzo zilizochukuliwa na CUF pia Chama Cha Mapinduzi (CCM) kunusuru hali ya kisiasa visiwani humo na kutaka majadiliano yaendelee.

Shekh Ponda amemshauri Rais John Magufuli kutimiza ahadi yake aliyoitoa bungeni ya kushughulikia mzozo huo kwa kushirikiana na Maalim Seif Shariff Hamad na Dk. Ali Mohammed Shein.

Amesema kuwa, Rais Magufuli hajatoa tamko lolote na kwamba hajaeleza amefikia wapi katika kutatua mzozo huu.

Sheikh Ponda amesema kuwa kuna viashiria vya kuvunjika kwa amani visiwani humo kutokana na watu kuporwa haki zao na kwamba watakapoamua kuitafuata kutazuka vurugu.

No comments: