Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni Yaunda Kanuni Zitakazowaongoza Wabunge Wake - LEKULE

Breaking

9 Feb 2016

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni Yaunda Kanuni Zitakazowaongoza Wabunge Wake



Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni (KUB) imeunda kanuni zitakazowaongoza wabunge wake kuendesha shughuli mbalimbali za chombo hicho cha uwakilishi.

Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema, Salum Mwalimu aliwaambia wanahabari jana kuwa kanuni hizo ambazo zimeundwa kwa kushirikisha vyama vyote vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) zitasaidia kuondoa holela iliyokuwa ikijitokeza awali ndani ya KUB.

Mwalimu, ambaye chama chake ndiyo kinaongoza kambi hiyo, alisema Chadema inaipongeza hatua hiyo kwa kuwa imeonyesha kuzaa matunda katika mkutano wa pili wa Bunge la 11 uliomalizika wiki iliyopita.

Kanuni hizo za kambi rasmi ya upinzani, kwa mujibu wa Mwalimu zimeanzishwa kwa kufuata kanuni ya 16, ibara ya 4 ya Kanuni za Kudumu za Bunge ambayo inasema:

“Vyama vya siasa vyenye uwakilishi bungeni vinaweza kutunga kanuni za vyama vya kwa ajili ya uendeshaji bora wa shughuli za vyama hivyo bungeni.”

Mwalimu alisema kanuni hizo tayari zimeshasaidia uteuzi wa wawakilishi katika vyombo vya kimataifa kupitia Bunge.

Alisema katika utaratibu wa kanuni hizo mpya jambo likishaamriwa kwenye vikao vya umoja huo hakuna mtu wa kupinga na ikitokea mbunge husika akazivunja hatua za kinidhamu zitachukuliwa. 

“Kwa sasa hamna tena songombingo ya kupata nafasi za uwakilishi ndani ya Bunge. Likipita jambo ndani ya caucus (kikao cha chama) basi limepita...hakuna tena kuvujisha siri ndiyo maana safari hii hata waandishi ilikuwa vigumu kupata taarifa za ndani,” alisema.

 Akizungumzia umeya Dar es Salaam alisema kuna hila za wazi za kutaka kuongeza wajumbe wasiotakiwa katika uchaguzi hasa kutoka Ilala na Kinondoni.

No comments: