Bodaboda Agonga Gari Na Kufariki Papo Hapo - LEKULE

Breaking

3 Feb 2016

Bodaboda Agonga Gari Na Kufariki Papo Hapo



DEREVA wa bodaboda, Colnery Mpande (18), mkazi wa Kiluvya Kwa Komba, amekufa baada ya pikipiki aliyokuwa akiiendesha kugonga gari kwa nyuma na yeye kuangukia barabarani na kukanyagwa kichwa na gari lingine.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Bonaventura Mushongi alisema pikipiki hiyo baada ya kuligonga gari hilo ilipoteza mwelekeo na kuanguka barabarani kisha kugongwa kwa kukanyagwa kichwa na kufa papo hapo.

Alisema tukio hilo ni la jana saa 10 alfajiri eneo la Mpakani, katika barabara ya Morogoro wilayani Kibaha.

Kamanda alisema gari aliloligonga kwa nyuma dereva huyo wa bodaboda lilisimama ghafla na halikuonesha ishara kwamba linakatisha kuingia kushoto.

Alisema Mpande alikuwa akiendesha pikipiki yenye namba za usajili MC 332 AXL aina ya Sanlg akitokea Kibaha kuelekea Kiluvya na aligonga gari lenye namba za usajili T 616 DCB aina ya Mitsubishi Canter lililokuwa likiendeshwa na Shaaban Ally kutoka Kibaha kwenda Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Kamanda, Mpande alikanyangwa kichwa na lori la mizigo lenye tela na namba za usajili T 559 BFA/T 874 AQF likiendeshwa na Daniel Joseph aliyekuwa akitokea Dar es Salaam kwenda Mbeya.

No comments: