Bei ya Mafuta Yashuka Tena - LEKULE

Breaking

3 Feb 2016

Bei ya Mafuta Yashuka Tena


Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), imetangaza bei kikomo ya mafuta, ambapo bei ya dizeli imeshuka kutoka Sh. 1,747 hadi Sh 1,600, likiwa ni punguzo la Sh. 147 kwa lita.

Kadhalika, bei ya mafuta ya petroli imeshuka kwa Sh. 55, hivyo kufanya mafuta hayo kuanzia leo kuuzwa kwa bei isiyozidi Sh. 1,842 kutoka Sh. 1,898 kwa lita kama kilivyokuwa ikiuzwa mwezi uliopita.

Taarifa iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, Felix Ngamlagosi, ilieleza kuwa, kupungua kwa bei ya mafuta kwenye soko la ndani  kwa kiasi kikubwa kumetokana na kushuka kwa bei ya nishati hiyo katika soko la dunia na pia kushuka kwa gharama za usafarishaji na bidhaa za mafuta hayo kuja nchini.

“Hakukuwa na mafuta ya taa yaliyoingizwa nchini Januari mwaka huu, hivyo Februari bei ya bidhaa hii itaendelea kuwa kama ilivyokuwa kwa Januari ambayo ni Sh. 1,699 kwa lita kwa soko la Dar es Salaam,”alisema.

Ngamlagosi alisema kushuka kwa namna hiyo kulitokea Machi, mwaka jana, lita moja ya mafuta ya dizeli ilishuka hadi kufikia Sh. 145 na dizeli kuzwa kwa Sh. 1,563 kwa lita.

Mkurugenzi huyo wa Ewura aliwaomba wananchi kupuuza uvumi unaoenezwa kuwa mamlka hiyo haipendi kushusha bei za mafuta kwa kuwa kushuka kwake kutaadhiri mapato.

Alisema tozo ya Ewura inatokana na kiasi cha lita za mafuta kinachouzwa na si kupanda kwa bei.

Aidha, amewakumbusha wamiliki wa vituo vyote vya mafuta kubandika bei za bidhaa za mafuta katika mabango yanayoonekana bayana, yakionyesha bei ya mafuta, punguzo, vivutio vya biashara na promosheni zinazotolewa na kituo husika.

No comments: