Serikali
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeamua kulifuta kutoka katika
Daftari la usajili wa magazeti, gazeti lijulikanalo kama “MAWIO”.
Amri
ya kulifuta Gazeti hilo imetolewa leo 17 Januari, 2016 na Waziri wa
Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Nape Nnauye wakati alipokutana
na Waandishi wa Habari katika Ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO)
uliopo Jijini Dar es Salaam.
Mhe.
Nnauye amesema kuwa kupitia Tangazo la Serikali Na. 55 lililotolewa
tarehe 15 Januari, 2016 Serikali imelifuta Gazeti hilo ikiwa ni uamuzi
uliotolewa kwa mujibu wa Sheria ya Magazeti Sura ya 229, kifungu 25(1).
Alieleza
kuwa, hatua ya kulifuta gazeti hilo inazuia pia gazeti la Mawio
kuchapishwa katika njia nyingine yoyote ikiwa ni pamoja na mitandao
(Online publication) kwa mujibu wa Sheria ya Mawasiliano ya Kieletroniki
na Posta Sura ya 306.
‘’Serikali
kwa masikitiko makubwa, imechukua uamuzi huu kutokana na mwenendo wa
uandishi wa gazeti hilo usioridhisha wa kuandika na kuchapisha habari
zenye mwelekeo wa uchochezi na kuhatarisha amani, utulivu na usalama wa
nchi yetu’’, alisema Nnauye.
Aidha,
alifafanua kuwa hatua hiyo ya kulifuta gazeti hilo imechukuliwa baada
ya Msajili wa Magazeti kufanya juhudi kubwa za muda mrefu kuanzia Juni,
2013 hadi Januari, 2016 kumtaka Mhariri wa gazeti hilo kubadili aina
ya uandishi wa habari na makala katika gazeti lake, bila mafanikio.
"Msajili
wa magazeti kwa juhudi zake alifanya mawasiliano na Mhariri wa gazeti
hilo mara nane kwa lengo la kutaka afanye marekebisho ya mtindo wa
kutoa habari zake lakini mhariri wa gazeti hilo hakuzingatia ushauri
mzuri aliopewa na Msajili wa Magazeti,
"Ninatoa
wito kwa wamiliki, wahariri, waandishi na watangazaji wa habari
kuzingatia sheria, Kanuni na taratibu za taaluma ya uandishi wa habari
ambazo zikizingatiwa hakutakuwa na migogoro yoyote.
"Aidha
Serikali inasisitiza kwamba inaheshimu uhuru wa vyombo vya habari
unaozingatia maadili, weledi na Sheria za nchi na kwamba Serikali
itaendelea kushirikiana navyo’’ alisisitiza Mhe. Nnauye.
Katika
hatua nyingine, Waziri nape alitoa pongezi kwa Vyombo vyote vya habari
nchini vinavyozingatia maadili, weledi na Sheria zinazosimamia taaluma
ya habari na sheria nyingine za nchi.
‘’Kwa
namna ya pekee Serikali inawapongeza wamiliki na wahariri wa vyombo vya
habari ambavyo vinapofanya makosa vikielekezwa hujirekebisha na kutoa
ushirikiano kwa Serikali na pia kubadili mwenendo wao; hawa ni pamoja
na wahariri wa magazeti ya; Mwananchi Tanzania, Mtanzania, The East
African, Magazeti ya Daily News na Habari Leo, Uhuru na mengineyo’’, alisema Mhe. Nnauye.
No comments:
Post a Comment