Waziri
wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga amesema katika kuhakikisha
Serikali inapambana na uhalifu, Jeshi la Polisi limeanza ukaguzi maalumu
wa bodaboda na kufunga kamera za CCTV katika miji mikuu ili kufuatilia
matukio mbalimbali.
“Kutokana
na majambazi kubuni mbinu mpya kila siku, ikiwamo ya kutumia bodaboda
kuvamia benki na wanaotoka benki na kuwapora fedha, kuanzia sasa
bodaboda, hasa aina ya boxer zitasimamishwa wakati wowote na
kupekuliwa,” alisema Kitwanga
Alisema
polisi wameweka ulinzi maalumu na waendesha bodaboda watakaooneka
kupakia kitu chochote na kukiweka mbele (katika tenki la mafuta) au kiti
cha nyuma, watasimamishwa na kupekuliwa kwa maelezo kuwa maeneo hayo
ndiyo hutumika kuficha silaha.
“Tunaomba wananchi watuvumilie kipindi hiki tukipambana na bodaboda kutokomeza uhalifu,” alisema.
Katika
miaka ya hivi karibuni, kumekuwa na matukio ya mara kwa mara ya
wananchi kuvamiwa na kuporwa fedha, ikiwa ni muda mfupi baada ya
kuzichukua benki huku wafanyakazi wa benki wakidaiwa kuhusika kutoa
taarifa za wateja.
Mara
zote majambazi hutumia bodaboda kufanikisha uhalifu huo, huku wakiwa na
silaha ambazo huzitumia kutishia, kujeruhi na wakati mwingine kuua.
Tukio
la hivi karibuni ni la Desemba 28 mwaka jana, ambako majambazi
waliokuwa katika bodaboda walimvamia meneja wa operesheni wa kampuni ya
simu za mkononi ya Zantel, Gabriel Raphael na kumpora Sh10 milioni na
kumuua kwa risasi.
Kuhusu ujambazi huo, Kitwanga alisema watu wanaovamiwa na kuporwa fedha, wengi hutokea katika benki za ndani si za nje.“...
Hii inatokana na utaratibu wa malipo katika benki hizi. Kwa mfano,
benki za nje ukiwa na hundi inapitiwa na watu wachache tofauti na benki
za ndani ambazo hupitiwa na watu wengi.”
“Inawezekana
katika mlolongo huo wa benki za ndani kukawa na wafanyakazi
wanaoshirikiana na majambazi. Tunachokifanya sasa ni kuongeza ulinzi tu
wa askari.”
Kuhusu
CCTV, Kitwanga ambaye pia ni mbunge wa Misungwi alisema teknolojia hiyo
itasaidia kubaini matukio ya uhalifu na kwamba tayari Serikali
imeshazungumza na China kuhusu upatikanaji wa kamera hizo, “Ufungaji wa utaanza mwaka ujao wa fedha unaoanza Julai na tutaanzia Dar es Salaam.”
Alisema
Jeshi la Polisi lina askari wachache ambao hawawezi kuwapo kila eneo,
hivyo mpango wa kuweka kamera hizo ni kuhakikisha kila jambo
linafuatiliwa kwa ukaribu.
“Wapo
waliokamatwa wakituhumiwa kuhusika katika matukio ya kuwapiga watu
risasi na kuwapora fedha. Baadhi yao wamekiri kuhusika na wengine
wamekana,” alisema Kitwanga.
Alipoulizwa silaha zinazotumika zinatoka wapi, alisema, “wanazopewa raia kihalali hazitumiki katika matukio haya. Ni zile zinazoingia nchini kinyemela.”
No comments:
Post a Comment