Walimu Wapigwa Marufuku Kupaka Wanja - LEKULE

Breaking

20 Jan 2016

Walimu Wapigwa Marufuku Kupaka Wanja


Serikali wilayani Geita  Mkoa wa Geita, imepiga marufuku walimu kuvaa mavazi yasiyolingana na taaluma yao na upakaji wanja na rangi ya mdomo kupita kiasi wanapokuwa kazini.

Ofisa Utumishi wa Wilaya ya Geita, Thabitha Bugema alitoa amri hiyo jana wakati akizungumza na walimu wakuu wa shule za msingi na waratibu elimu kwenye kikao cha muongozo wa kutumia fedha za elimu bure zilizotolewa na Serikali.

Bugema alisema baadhi ya walimu wanavaa mavazi ya upotoshaji ambayo hayaendani na ya ofisini.

Alisema walimu wa kiume huvaa suruali za jeans, fulana zenye nembo ya timu za mpira na wengine kuvaa mlegezo na kunyoa nywele mitindo isiyo ya heshima.

“Nashindwa kuelewa wapo walimu wanavaa kama wauza baa, amejipaka lipstick (rangi ya mdomo) na wanja kama anakwenda kwenye kumbi za muziki usiku, wakuu wa shule sitegemei kuwaona mkifumbia macho walimu wa aina hiyo,” alisema Bugema

Alisema kila mtumishi wa Serikali anafahamu mavazi ya ofisini na kuwataka walimu kubadilika na kuvaa mavazi ya heshima yanayoendana na taaluma yao.

Ofisa Elimu Msingi Wilaya ya Geita, Deus Seif alisema wamepokea Sh80 milioni kwa ajili ya elimu bure na kuwataka wakuu wa shule kuhakikisha zinatumika kama ilivyopangwa.

Mkuu wa wilaya hiyo, Manzie Mangochie aliwataka walimu na waratibu elimu kufanya mikutano ya wazazi ya kuwaelimisha maana ya elimu bure na kuwaeleza mambo ambayo Serikali inafanya na wajibu wa wazazi kwa watoto wao.   

No comments: