Taarifa ya Uteuzi wa Wabunge Kwenye Kamati za Kudumu Za Bunge - LEKULE

Breaking

12 Jan 2016

Taarifa ya Uteuzi wa Wabunge Kwenye Kamati za Kudumu Za Bunge


TAARIFA KWA UMMA KUHUSU UTEUZI WA WABUNGE KWENYE KAMATI ZA KUDUMU ZA BUNGE.

Katibu wa Bunge anatoa taarifa kwa umma kwamba:


(a) Kwa mujibu wa Kanuni ya 116 (3) ya Kanuni za Kudumu za Bunge, Toleo la Aprili, 2013, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano amepewa mamlaka ya kuteua Wajumbe wa Kamati za Kudumu za Bunge kwa namna ambayo itawezesha kila Mbunge kuwekwa kwenye Kamati mojawapo. Katika kufanya uteuzi huo, Spika huzingatia vigezo mbalimbali vilivyoainishwa katika Kanuni ya 116 (5);

(b) Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Mhe. Job Yustino Ndugai (MB), ametekeleza mamlaka yake ya uteuzi kwa mujibu wa Kanuni tajwa hapo juu, kwa kuwateua kwanza Wabunge Kumi na Tano (15) kuwa Wajumbe wa Kamati ya Kanuni za Bunge.

 Kamati hiyo imeundwa na kutangazwa kabla ya Kamati zingine ili ifanye marekebisho ya Nyongeza ya Nane ya Kanuni za Kudumu za Bunge kuhusu majukumu ya Kamati zingine za Bunge kwa kuyashabihisha na majukumu ya Serikali kwa kuzingatia Muundo wa Baraza la Mawaziri lililopo sasa.

 Lengo kuu ni kuleta urahisi, ufanisi na tija kwa Bunge katika kuisimamia na kuishauri Serikali;

(c) Kwa msingi huo, Kamati ya Kanuni za Kudumu za Bunge, ambayo Spika ndiye Mwenyekiti wake na Naibu Spika ni Makamu Mwenyekiti, Kiongozi wa Upinzani na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambao ni Wajumbe kwa nyadhifa zao itakutana katika Ofisi ya Bunge, Dar es Salaam siku ya Ijumaa tarehe 15 Januari, 2016 saa tano kamili asubuhi katika Ukumbi wa Spika. Wajumbe wengine ni: -
 
(i) Mhe. Makame Kassim Makame, MB. - Jimbo la Mwera;

(ii) Mhe. Tundu Antipas Mughwai Lissu, MB. - Jimbo la Singida Mashariki;

(iii) Mhe. Jasson Samson Rweikiza, MB. - Jimbo la Bukoba Vijijini;

(iv) Mhe. Ally Saleh Ally, MB. - Jimbo la Malindi;

(v) Mhe. Magdalena Hamis Sakaya, MB. - Jimbo la Kaliua;

(vi) Mhe. Salome Wycliff Makamba, MB. - Viti Maalum;

(vii) Mhe. Dkt. Jasmine Tiisekwa Bunga, MB. - Viti Maalum;

(viii) Mhe. Zainab Athman Katimba, MB. - Viti Maalum;

(ix) Mhe. Balozi Adadi Mohamed Rajab, MB. - Jimbo la Muheza;

(x)Mhe. Dkt. Charles John Tizeba, MB. - Jimbo la Buchosa; na

(xi) Mhe. Kangi Alphaxard Lugola, MB. - Jimbo la Mwibara.

(d) Spika atakamilisha uteuzi wa Wajumbe katika Kamati zingine za Bunge kabla ya kuanza kwa Mkutano wa Pili wa Bunge tarehe 26 Januari, 2016, Mjini Dodoma ili kutoa fursa kwa Kamati zote kuchagua Viongozi wake na kuandaa Mpango Kazi kwa mwaka 2016/17; na

(e) Wabunge wote wanatangaziwa kuwa wawe wamefika Dodoma tarehe 20 Januari, 2016 tayari kwa kuanza kwa Kamati za Bunge na Mkutano wa Bunge, isipokuwa Kamati ya Wabunge (Caucus) wote wa Chama cha Mapinduzi wanatakiwa kuwa Mjini Dodoma tarehe 17 Januari, 2016 kwa Mkutano wao.

Imetolewa na:
Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano,
Ofisi ya Bunge,
S. L. P. 9133,
DAR ES SALAAM.
11 Januari, 2016.

No comments: