Wazanzibari Kusherehekea Miaka 52 ya Mapinduzi LEO - LEKULE

Breaking

12 Jan 2016

Wazanzibari Kusherehekea Miaka 52 ya Mapinduzi LEO


WAZANZIBARI leo wanasherehekea miaka 52 ya Mapinduzi ya Januari 12 mwaka 1964, ambayo yaling’oa utawala wa Sultani kutoka Oman na kuwezesha wazalendo wengi kushika hatamu ya kuongoza nchi.

Katika kilele cha sherehe hizo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Ali Mohamed Shein atahutubia taifa katika uwanja wa Amaan.

Atapokea maandamano ya wananchi wa mikoa mitano ya Unguja. Matukio mengine makubwa yatakayofanyika katika uwanja huo ni Rais Shein kukagua gwaride la heshima la vikosi ya ulinzi na usalama, vikiongozwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) .

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na idara ya sherehe na mapambo iliyo chini ya Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, sherehe hizo zitahudhuriwa na viongozi wa ngazi za kitaifa akiwemo Rais wa Jamhuri ya Muungano, John Magufuli ambaye ni mara ya kwanza kushiriki baada ya kuchaguliwa katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 25 mwaka jana.

Ratiba hiyo inaonesha kwamba sherehe hizo, zitahudhuriwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa na marais wastaafu wa Jamhuri ya Muungano na wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Akizungumza na waandishi wa habari, Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kusherehekea miaka 52 ya Mapinduzi, yaliyowakomboa wakulima na wafanyakazi kutoka katika kucha za wakoloni wa kisultani.

Aliwapongeza wananchi kwa kujitokeza na kushiriki katika ufunguzi wa miradi ya maendeleo, ambayo malengo yake ni kuharakisha maendeleo na kupambana na umasikini.


Mitaa mbalimbali mjini hapa, imepambwa picha za viongozi mashuhuri waliosimama kidete kufanya Mapinduzi hayo; hususan Rais wa Kwanza, Abeid Amaan Karume aliyeongoza timu ya watu 16 kufanya mapinduzi hayo.

No comments: