Rais Uhuru Kenyatta akihutubia taifa baada ya mkasa wa mauaji dhidi ya wanajeshi wa nchi hiyo kusini magharibi mwa Somalia.
Miili ya
wanajeshi wa Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF) waliouwawa nchini Somalia
imepokelewa kwa heshima zote za kijeshi nchini Kenya huku operesheni
kubwa ya kuwakomboa wenzao walionusurika ikiendelea.
Waziri wa
Ulinzi wa Kenya, Raychelle Omamo, ndiye aliyeongoza ujumbe wa serikali
katika kuzipokea maiti za wanajeshi hao zilipowasili kwenye uwanja wa
ndege jijini Nairobi huku pia kukifanyika utaratibu maalum wa kutoa
heshima za kijeshi.
Akizungumza
kwa huzuni kubwa, Omamo aliwaomba Wakenya waendelee kuwa na subira
wakati shughuli za kuwakomboa wanajeshi wengine zikiendelea. Alisema pia
juhudi za kuipata miili zaidi ya wanajeshi waliouwawa zinaendelea ili
nayo irejeshwe nyumbani kwa mazishi rasmi.
''Huu ni
wakati wa majonzi kwa Jeshi la Kenya na kwa taifa letu kwa ujumla. Kwa
mara nyingine, tungependa kutoa shukurani zetu kwa Wakenya wanaotuunga
mkono kwa upendo wao katika kipindi hiki kigumu, kwa wanajeshi wetu na
familia zao. Kama nilivyowaeleza awali, shughuli ya kuwatafuta na
operesheni ya uokozi zinaendelea na tunatarajia kuwapokea wanajeshi wetu
zaidi kadri siku zinavyokwenda.''
Hata
hivyo, waziri huyo wa ulinzi hakutoa idadi kamili ya wanajeshi wa KDF
waliouwawa, ingawa ameweka wazi kwamba wanategemea maiti zaidi. Kambi ya
Jeshi la Umoja wa Afrika (AMISOM) kusini magharibi mwa Somalia
ilishambuliwa na wapiganaji wa al-Shabaab mapema Ijumaa, likiwa ni tukio
la hivi karibuni kabisa kwa AMISOM kushambuliwa ndani ya Somalia.
Al-Shabaab yadai kuuwa wanajeshi 100
Licha ya
serikali ya Kenya kutosema idadi ya wanajeshi wake waliouwawa,
kujeruhiwa au kutoweka, siku ya Jumapili kundi hilo la al-Shabaab
lilitoa taarifa likisema zaidi ya wanajeshi 100 wa Kenya waliuwawa na
wengine kushikiliwa mateka.
Katika
taarifa yake, Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya alisema kundi hilo halitopata
muda wa kupumua, huku akiapa kwamba nchi yake italipiza kisasi ingawa
haijafahamika hadi wakati huu ikiwa wanajeshi wa KDF walioko Somalia
wameifikia kambi hiyo inayoshikiliwa na wanamgambo wa al-Shabaab.
Kadhalika,
al-Shabab limetoa kanda mbili za sauti zilizorekodiwa likidai wanajeshi
kadhaa wanashikiliwa mateka, na tovuti zao ndani ya Somalia zikitaja
wanajeshi 12 kuwa ndio wanaoshikiliwa.
Waziri
Mkuu wa Somalia, Omar Abdirashid Sharmake, amelaani mashambulizi hayo
akisema ni kitendo cha kinyama huku pia akituma salamu za rambirambi kwa
familia za wanajeshi waliouwawa.
Umoja wa
Ulaya, ambao ni mfadhili mkubwa wa kikosi cha AMISOM, umelaani pia
mashambulizi hayo ukisema ni "jaribio jingine la kuuhujumu mchakato wa
kisiasa kuelekea Somalia thabiti yenye usalama."
No comments:
Post a Comment