Uswis
iimeahidi kuendeleza ushirikiano na Tanzania katika Nyanja mbalimbali
za maendeleo huku mkazo mkubwa ukiuelekeza katika kuendeleza elimu ya
mafunzo ya ufundi stadi.
Balozi
wa Uswisi hapa Nchini Mheshimiwa Florence Tinguelly Mattli, amesema
hayo leo tarehe 23 Desemba, 2015 alipokutana na kufanya mazungumzo na
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli Ikulu
Jijini Dar es salaam.
Balozi
Florence amemueleza Rais Magufuli kuwa pamoja na kuwepo kwa miradi
mingine ambayo nchi hiyo inaendelea kuitekeleza kwa kushirikiana na
Tanzania, katika awamu hii Uswisi itatilia mkazo katika elimu ya ufundi
stadi ilikuwawezesha vijana wanaosoma kuwa na ujuzi unaowawezesha
kuzalisha bidhaa na kujipatia kipato kama ambavyo nchi ya Uswisi
inafanya.
Maeneo
mengine ambayo viongozi hao wamezungumzia nikuimarisha ushirikiano
katika uwekezaji, ambapo Rais Magufuli amewaalika wawekezaji kutoka
Uswisi kufanya biashara na Tanzania, kuimarisha huduma za bandari na pia
kuongeza uwezo katika kukabilia na na vitendo vya Rushwa.
Kuhusu
Sekta ya afya, Rais Magufuli ameipongeza Uswisi kwa kushirikiana na
Tanzania kupitia Taasisi ya Afya Ifakara katika kukabiliana na
changamoto mbalimbali za kiafya ikiwemo kukabiliana na ugonjwa wa
Malaria na ameahidi kuwa Serikali itaendelea kuitumia taasisi hiyo
ilikusaidia juhudi za kukabiliana na magonjwa.
Wakati
Huo Huo, Rais wa Jamhuri ya Muunganowa Tanzania Dkt. John Pombe
Magufuli amekuta na nakufanya mazungumzo na Balozi wa Kuwait hapa Nchini
Mheshimiwa Jasem Al Najem Ikulu, Jijini Dar es salaam.
Katika
Mazungumzo hayo, Balozi Al Najem amewasilisha salamu za mfalme wa
Kuwait Mheshimiwa Sabah Al Ahamad Al Jaber al Sabah kwa Rais Magufuli,
ambaye amempongeza kwa kuchaguliwa kuwa Rais waawamu ya tano na
amemhakikishia kuwa Kuwait itaendelea kushirikiana na Tanzania katika
maendeleo ikiwemo kufadhili utekelezaji wa miradi mbalimbali katika
sekta za ujenzi, Maji na Kilimo.
Miongoni
mwa miradi hiyo ni mradi wa ujenzi C wa barabara ya Chaya – Nyahua
yenye urefu wakilometa 85 kwa kiwango cha lami ambapo Tanzania imeomba
ufadhili wa dola milioni 85, Mradi wa Maji wa Same - Mwanga – Korogwe
ambapo Tanzania imeomba ufadhili wa dola milioni 20 na Mradi mkubwa wa
kilimo cha umwagiliaji katika bonde la Mhongo na Luhiche Mkoani Kigoma
ambapo Kuwait imeonesha nia ya kuufadhili.
Aidha,
Rais Magufuli amemshukuru Mfalme wa Kuwait kwa salamu zake za pongezi
na amewaalika wafanyabiashara wa Kuwait kushirikiana na Tanzania katika
biashara na uwekezaji.
Katika
Hatua nyingine Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe
Magufuli amekutana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda Mheshimiwa Louise
Mushikiwabo aliye tumwa kuleta ujumbe maalum wa Rais Paul Kagame wa
Rwanda.
Katika
Ujumbe huo, Mheshimiwa Kagame amemuhakikishia Rais Magufuli kuwa Rwanda
itaendelea kushirikiana na Tanzania katika Nyanja mbalimbali za
kiuchumi, kisiasa na kijamii hasa ikizingatiwa kuwa licha ya kuwa ni
nchi jirani ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Rwanda ni marafiki na
ndugu wa Tanzania.
Rais
Kagame pia amempongeza Rais Magufuli kwa uongozi mzuri aliouonesha
katika siku za mwanzo za uongozi wake wa awamu ya tano ambao amesema
anauunga mkono.
Pamoja
na kupokea salamu za Rais Kagame, Rais Magufuli na Waziri wa Mambo ya
Nje wa Rwanda wamezungumzia mgogoro wa kisiasa unaoendelea nchini
Burundi na wote kwa pamoja wameona nimuhimu kupata suluhisho kwa njia ya
mazungumzo ili wananchi waweze kuishi kwa amani na kuendelea na
shughuli zao za maendeleo
Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es salaam
23 Desemba, 2015
Rais
Dkt John Pombe Joseph Magufuli akizungumza na balozi wa Kuwait hapa
nchini Mhe. Jasem Al Najem Ikulu jijini Dar es salaam leo Disemba 23,
2015
Rais
Dkt John Pombe Joseph Magufuli akimsindikiza balozi wa Kuwait hapa
nchini Mhe. Jasem Al Najem baada ya kuwa na mazungumzo naye Ikulu jijini
Dar es salaam leo Disemba 23, 2015.
Rais
Dkt John Pombe Joseph Magufuli akisalimiana na Mjumbe Maalum wa Rais
Paul Kagame wa Rwanda ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo
Mhe. Louise Mushikwabo Ikulu jijini Dar es salaam leo Disemba 23, 2015
Rais
Dkt John Pombe Joseph Magufuli akizungumza na Mjumbe Maalum wa Rais Paul
Kagame wa Rwanda ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo Mhe.
Louise Mushikwabo Ikulu jijini Dar es salaam leo Disemba 23, 2015.
Rais
Dkt John Pombe Joseph Magufuli akimsindikiza Mjumbe Maalum wa Rais Paul
Kagame wa Rwanda ambaye pia ni Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo Mhe.
Louise Mushikwabo Ikulu jijini Dar es salaam leo Disemba 23, 2015. Nyuma
yao ni Balozi wa Rwanda nchini.
No comments:
Post a Comment