TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA - TAMISEMI
TAARIFA KWA
VYOMBO VYA HABARI
Ndugu
wanahabari nimewaita hapa leo ili mnisaidie kufikisha ujumbe kwa
wananchi kuhusu mradi wetu wa Mabasi yaendayo Haraka katika Jiji la Dar
es Salaam (DART – BRT).
Kama
mnavyofahamu Serikali ilianzisha mradi huu ili kupunguza msongamano wa
magari barabarani kwa madhumuni ya kurahisisha usafiri na usafirishaji
katika Jiji letu.
Kutokana
na kukamilika kwa sehemu ya ujenzi wa miundombinu ya Awamu ya Kwanza ya
mradi, Serikali iliamua tuwe na mtoa huduma wa mpito (Interim Service
Provider) kabla ya kumpata mtoa huduma wa kudumu (Service Provider).
Mtoa
huduma wa mpito alipaswa kupatikana kwa mujibu wa Sheria ya Manunuzi ya
Umma. Hata hivyo, Serikali imebaini ukiukwaji wa wazi wa sheria hiyo
wakati wa kumpata mtoa huduma wa kipindi cha mpito.
Kufuatia hali hiyo nimeamua kumsimamisha kazi kuanzia leo tarehe 23 Desemba, 2015, Mtendaji Mkuu wa DART, Bi. Asteria Mlambo ili kupisha uchunguzi.
Sababu za kumsimamisha kazi ni:
i. Kushindwa kuzingatia Sheria ya Manunuzi ya Umma wakati wa kumpata mtoa huduma katika kipindi cha mpito;
ii.
Kushindwa kuchukua hatua hata pale alipobaini kuwa mtoa huduma wa mpito
amekiuka masharti ya mkataba wa kutoa huduma ya mpito; na
iii. Kufanya maamuzi makubwa pasipo kuishirikisha Bodi ya Ushauri ya DART.
Aidha,
Serikali inatambua kuwa wapo watumishi wa DART ambao hawakumshauri
vizuri Mtendaji Mkuu. Watumishi hao watachunguzwa na kuchukuliwa hatua
na Kaimu Mtendaji Mkuu atakayeteuliwa.
Nimemwagiza Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI kuendelea na taratibu za kinidhamu dhidi ya Mtendaji Mkuu aliyesimamishwa kazi.
Naitumia
nafasi hii kuwahakikishia kuwa Serikali itaendelea kuchukua hatua kwa
haraka na uangalifu ili mradi huu uweze kuanza kutoa huduma bora ya
usafiri kwa wakazi wa Dar es salaam bila kuchelewa zaidi. Aidha, natoa
rai kwa wananchi kuitunza na kuithamini miundombinu ya DART kwa kuwa
imegharimu fedha nyingi kwa manufaa yao.
Imetolewa na:-
George B. Simbachawene,
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI
No comments:
Post a Comment