Rais Magufuli Afanya Mazungumzo Na Spika Wa Baraza La Seneti Na Mjumbe Maalum Wa Rais Wa Jamhuri Ya Burundi,pierre Nkurunzinza - LEKULE

Breaking

23 Dec 2015

Rais Magufuli Afanya Mazungumzo Na Spika Wa Baraza La Seneti Na Mjumbe Maalum Wa Rais Wa Jamhuri Ya Burundi,pierre Nkurunzinza


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amekutana na kufanya mazungumzo na Spika wa  Seneti na Mjumbe Maalum wa Rais wa Jamhuri ya Burundi Mheshimiwa Reverien Ndikuriyo Ikulu jijini Dar Es Salaam kuhusu  hali ya kisiasa na usalama nchini Burundi na jitihada zinazochukuliwa na Tanzania ikiwa ni Mwenyekiti wa Jumuia ya Afrika Mashariki

Akiwasilisha ujumbe wa Rais Pierre Nkurunzinza wa Burundi kuhusu hali ya Burundi, Spika Ndikuriyo amesema Serikali ya Burundi ipo tayari kufanya mazungumzo na wadau wote wa siasa kuhusu hali ya Burundi na jitihada za kuumaliza mgogoro wa kisiasa unaoendelea nchini humo

Akitoa maelezo ya kikao hicho kwa niaba ya Rais Magufuli, Balozi Maiga amesema serikali ya Burundi imekubali usuluhishi unaofanywa na Rais wa Uganda Mh. Yoweri Kaguta Museveni kwa niaba ya Marais wa Jumuia ya Afrika Mashariki kutokana na kikao kilichofanyika Jijini Dar es salaam mwezi Julai mwaka huu na kwamba serikali ya Burundi iko tayari kushiriki katika mazungumzo hayo ya amani.

“Mheshimiwa Rais Magufuli amefanya mazungumzo na rais Pierre Nkurunzinza wa Burundi mwishoni mwa wiki iliyopita ambaye amemuhakikishia Rais Magufuli utayari wake wa kushiriki katika mazungumzo hayo ya usuluhishi” Alisema Balozi Maiga .

Balozi Maiga ameongeza kuwa “nimeagizwa nilipeleke taarifa kwa mawaziri wa nchi za nje wa nchi jirani juu ya maandalizi ya mazungumzo hayo ambayo yataanza kule Uganda tarehe 28 mwezi Desemba na Waziri wa Ulinzi wa Uganda amekabidhiwa jukumu la kuratibu mazungumzo hayo”

Ameongeza kuwa suala jingine lililojitokeza katika mazungumzo hayo ni juu ya uamuzi wa baraza la usalama la umoja wa Afrika kutaka kupeleka majeshi yake nchini Burundi baada ya siku tano jambo ambalo Bunge la Burundi limepinga.

Balozi Mahiga amesema Burundi imepinga maamuzi hayo kwa kuwa inaamini kuwa hakuna hali ama dalili za kutokea kwa mauaji ya kimbari kama ya Rwanda, na kwamba kwa sasa kuna utulivu nchini humo tofauti na wasiwasi wa Umoja wa Afrika, Jumuia za kimataifa hasa Umoja wa Ulaya, na kwa kiwango fulani Umoja wa Mataifa unaotoa msukumo wa kutaka kuyapeleka majeshi ya kulinda amani nchini Burundi.

“Wao kama Burundi wakiwa ni washirika wakubwa wa kulinda amani katika bara la Afrika wana wanajeshi 6000 nchini Somalia,wanajeshi 1000 Jamhuri ya Afrika ya Kati na dhamira yao katika kushiriki kuleta amani, wao watakuwa ni watu wa mwisho kuleta hali itakayosababisha hatari ya kutokea kwa mauaji yanayofanana na mauaji ya kimbari” amesisitiza Balozi Mahiga

Dkt. Maiga amesema kutokana na maelezo hayo, Rais Magufuli amependekeza kuwa serikali ya Burundi ifungue milango ya mazungumzo na kuwakaribisha Umoja wa nchi za Kiafrika kupeleka ujumbe wa aina yeyote ili kwa pamoja waweze kutathmini hali usalama ilivyo nchini Burundi badala ya kukataa pendekezo hilo moja kwa moja.

Aidha, Balozi Mahiga amesema, Rais Magufuli amemuagiza kwenda nchini Burundi kutazama, kujiridhisha na kutathmini hali halisi ilivyo hususani katika suala la amani hasa ulinzi na usalama wa raia katika jiji la Bujumbura na maeneo mengine ya nchi hiyo ili kufahamu sababu zinazowafanya warundi kukimbia nchi yao na kukimbilia nchi majirani ikiwemo Tanzania kama wakimbizi.

Ameongeza kuwa safari yake ya kwenda Burundi kwa kiasi kikubwa itasaidia katika kuendeleza mazungumzo yanayotarajia kufanyika huko Uganda.

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU.
Dar es Salaam.

22 Desemba, 2015

No comments: