Muhongo Achoshwa na Umeme wa Bei ya Juu Unaonunuliwa Uganda - LEKULE

Breaking

28 Dec 2015

Muhongo Achoshwa na Umeme wa Bei ya Juu Unaonunuliwa Uganda


Waziri wa wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo ameuagiza uongozi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Kanda ya Ziwa kuhakikisha wanauingiza mkoa wa Kagera katika Gridi ya Taifa baada ya kubainika nchi inaingia gharama kubwa kununua umeme kutoka Uganda.

Alitoa agizo hilo jana wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Kagera na kusisitiza katika mipango mipya ya Tanesco kwa sasa, ni lazima iondokane na umeme wa gharama kubwa.

Katika ziara hiyo ambayo alikagua mitambo ya kusambaza umeme katika wilaya za Bukoba, Biharamulo na Ngara, Muhongo alisema umeme unaonunuliwa kutoka Uganda wa megawati 5.2 , kila uniti hununuliwa senti nane za Kimarekani.

Aliagiza kwamba kabla ya Tanesco kusaini mkataba mpya na Uganda, wanapaswa kusaini mkataba wa muda wakati wakiendelea kuweka utaratibu wa kuhamishia mkoa wa Kagera kwenye Gridi ya Taifa. Alisema mkoa huo ukiingizwa kwenye gridi, Tanesco itaepuka gharama kubwa za kunununua umeme wa gharama ya juu kutoka nchi hiyo.

Alisema kwa sasa Gridi ya Taifa imefika Nyakanazi, wilayani Biharamulo. “Kwa hiyo hata wilaya nyingine hazina budi kuingizwa katika gridi ili kufanya mkoa uwe na umeme wa uhakika na wa bei nafuu utakaowafanya wananchi kuzalisha kwa kutumia umeme…,” alisema.

Alisema Tanzania lazima iwe na umeme wa uhakika na wa gharama nafuu ndipo itafikia malengo ya nchi ya kipato cha kati. Alisisitiza kuwa, bila umeme, viwanda haviwezi kuzalisha na ajira haziwezi kupatikana. Alisema hakuna nchi yoyote duniani ambayo ina kipato cha kati ambayo watu wa kati hawatumii umeme.

Alisema Tanzania ina asilimia 42 wakati inatakiwa kufikia asilimia 75. “Kwa hiyo Tanesco mtake msitake, lazima umeme uwepo tena wa bei nafuu ili kuwezesha viwanda vyetu viweze kuzalisha kwa wingi na pato letu liweze kupanda zaidi ya mara nne na asiyetaka kasi hiyo ataondoka atuachie kazi zetu,” aliagiza Muhongo.

Wakati huo huo, aliagiza uongozi wa Tanesco wilaya ya Biharamulo kwamba ifikapo Januari 2 mwakani, wawapatie majibu wananchi wa kata ya Nyarukongongo yenye kaya 800 ni lini watapatiwa umeme. Alisema wameshachangia fedha zao na wanahitaji umeme.

Alisisitiza, wakati huu sio wa kusubiri wateja wawafuate maofisa wa Tanesco ofisini bali wao wanapaswa kuwafuata wateja vijijini. Aliwataka Tanesco kuacha tabia ya kuomba fedha Hazina wakati zipo kwa wananchi wanaohitaji kuunganishiwa umeme.

Aidha, ameagiza uongozi wa Tanesco mkoani Kagera kuhakikisha wanafunga umeme katika jengo la Forodha la Rusumo kwa upande wa Tanzania ndani ya wiki moja ijayo na kuepuka hali ya sasa ambayo watumishi wanatumia umeme kutoka Rwanda.

Meneja wa Tanesco wa Kanda ya Ziwa, Aron Maganga alimweleza Waziri Muhongo kuwa ifikapo mwaka 2018, mradi wa Gridi ya Taifa utakuwa umekamilika katika mkoa wa Geita na itakuwa rahisi mkoa wa Kagera kuingizwa kwenye gridi hiyo.

Maganga alisema chini ya mpango wa sasa, shirika limetoa maagizo kwa mameneja wote wa Mikoa na Wilaya kuhakikisha ifikapo Januari 15 mwakani mita mbovu zote zitarekebishwa na wateja wote wa zamani walioomba kuunganishiwa umeme watakuwa wameunganishiwa umeme.

Waziri aliwataka wananchi hao kuwa ifikapo Janurai 15, matatizo hayo ya kufungiwa umeme na uwapo wa mita mbovu katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Kagera, watoe taarifa kwa wakuu wa wilaya matatizo yao yashughulikiwe.

Waziri Muhongo ametembelea vituo vya kupokea na kusambaza umeme vya kuzalisha umeme vya Kibeta, Biharamulo, Ngara na kukagua jengo la forodha la Rusumo na mradi wa kuzalisha umeme wa maji wa Rusumo.
 Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kulia) akimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Kagera, John Mongella kabla ya kuanza ziara ya kukagua miundombinu ya umeme mkoani humo.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (wa pili kushoto) akimsikilizaMhandisi Filbert Mlaki.

Waziri wa nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo (kushoto) akikagua moja ya mtambo wa kuzalisha umeme wa Kituo cha Kibeta

No comments: