Lipumba Amtwika Zigo Dr Shein Mgogoro Zanzibar....Asema Mgogoro Utakwisha Iwapo Dr Shein Atakubali ZEC Iendelee Kutangaza Matokeo - LEKULE

Breaking

31 Dec 2015

Lipumba Amtwika Zigo Dr Shein Mgogoro Zanzibar....Asema Mgogoro Utakwisha Iwapo Dr Shein Atakubali ZEC Iendelee Kutangaza Matokeo


Mwenyekiti wa zamani wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amesema Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein ndiye mtu pekee mwenye uwezo wa kumaliza mgogoro wa Zanzibar.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Profesa Lipumba alisema mgogoro wa Zanzibar utamalizwa kwa Dk Shein kuiruhusu Tume ya Uchaguzi wa Zanzibar (ZEC) kutangaza matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25.

Alisema pamoja na mazungumzo yanayoendelea kati ya CUF na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Dk Shein ndiye mwenye uwezo kuumaliza mgogoro huo.

“Mazungumzo yanaendelea na hatujui yatafika mwisho lini, lakini Dk Shein ndiye anayeweza kuifanya Zanzibar iwe na amani au vurugu, ninashauri aruhusu kutangazwa kwa matokeo,” alisema.

Alisema amani na utulivu uliopo Zanzibar wakati wananchi wakisubiri hatima ya mgogoro huo, haiwezi kuwa ya kudumu kwani ikiamuliwa uchaguzi urudiwe wapo ambao hawatakubali.

Profesa Lipumba alisema uchaguzi wa Zanzibar ulikuwa huru na haki na hata watazamaji wa kimataifa kutoka nchi mbalimbali walishangaa matokeo yake kufutwa.

Alisema wananchi wa Zanzibar walishapiga kura na kwamba wanachosubiri ni matokeo vinginevyo haki yao ya kidemokrasia itakuwa imechezewa.

Oktoba 28 mwaka huu, Mwenyekiti wa ZEC, Jecha Salim Jecha alifuta uchaguzi huo kwa kile alichosema kulikuwa na kasoro ndani ya tume yenyewe na kwenye vituo vya kupigia kura.

Profesa Lipumba alisema mgogoro huo ukiendelea, utakwamisha msaada wa Dola za Marekani 472.8 milioni uliokuwa utolewe na Shirika la Maendeleo ya Milenia (MCC) la Marekani.

Alisema Bodi ya MCC ilikutana Desemba 16 na kushindwa kupitisha msaada huo kwa Tanzania huku hoja kubwa ikiwa kufutwa kwa matokeo ya Uchaguzi Mkuu Zanzibar.

Alisema miongoni mwa matumizi ya msaada huo ilikuwa kuunganisha wateja wapya 300,000 kupata umeme.

“Hapa tunategemea busara za Dk Shein kuumaliza mgogoro ili tupate msaada huo wenye masilahi ya Taifa au kuendelea na mgogoro na kuukosa msaada huo,” alisema.

Akizungumzia suala hilo, Naibu Katibu Mkuu wa CUF (Bara), Magdalena Sakaya alisema huu ni muda mwafaka kwa Dk Shein kuweka masilahi ya Wazanzibari mbele.

Alisema atawekwa kwenye vitabu vya historia kama atafanya uamuzi wa kuruhusu kutangazwa kwa matokeo hata kama viongozi wenzake wa CCM hawatapenda uamuzi huo.


“Lakini vurugu zikitokea, Shein atalaumiwa jumuiya za kimataifa yeye mwenyewe na atashangaa viongozi wenzake wa CCM watakapojiweka pembeni,” alisema.   

No comments: