Kiama cha Wafanyakazi Waliosafiri Nje Ya Nchi chaja - LEKULE

Breaking

28 Dec 2015

Kiama cha Wafanyakazi Waliosafiri Nje Ya Nchi chaja


Adhabu inawanyemelea watumishi wa serikali waliokaidi agizo la kutosafiri nje ya nchi bila kibali cha Rais John Magufuli na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue.

Habari zilizopatikana kutoka baadhi ya wizara  zilieleza jana kuwa tayari baadhi ya Makatibu Wakuu wa Wizara wameshapewa orodha ya majina ya watumishi waliosafiri nje ya nchi kinyemela.

Chanzo kimoja cha habari kimesema  kuwa tayari majina hayo yamepatikana na kinachofanyika sasa ni kupitia taratibu, sheria na kanuni kabla ya kuwachukulia hatua.

Watumishi wanne wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) wamesimamishwa kazi kwa kwenda nje ya nchi licha ya maombi yao ya kusafiri kukataliwa na mamlaka.

Jana   Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Ustawi wa Jamii, Wazee na Watoto, Dk. Donald Mmbando  alikiri kukabidhiwa taarifa kuhusu watumishi waliosafiri nje ya nchi bila kibali cha Ikulu na kwamba kwa sasa kuna taratibu ambazo zinafanyiwa kazi na ngazi husika kwa ajili ya kuchukua hatua zaidi.

“Ni kweli niliagiza nipatiwe taarifa ya watumishi hao na nimeshapewa ila kuna tataribu ambazo zinafanyiwa kazi na zitakapokamilika itatolewa taarifa ya wale wote waliosafiri na wamefanywa nini,” alisema Dk. Mmbando.

“Kwa sasa siwezi kulizungumzia ila likikamilika tutawajulisha.” Hivi karibuni Dk. Mmbando alitoa taarifa kwa wakuu wa Idara wizarani kwake akiwataka ifikapo Desemba 21 awe amepata taarifa ya wale wote waliokiuka agizo la Rais la kutosafiri nje ya nchi.

Dk. Mmbando aliandika dokezo kwenda kwa wakuu wa idara hiyo ambayo iliwataka kuwataja watumishi walio chini yao ambao walisafiri nje ya nchi baada ya katazo la Rais Dk. Magufuli.

Katika dokezo hilo walitakiwa kueleza watumishi hao wamesafiri kuelekea nchi gani, tarehe ya safari, madhumuni ya safari hizo, safari hizo zimegharamiwa na nani pamoja na kiasi cha fedha kilichotumika.

Waliosimamishwa kazi Takukuru ni Msemaji Doreen Kapwani, Mary Mosha, Ekwabi Mujungu na Rukia Nikitas. 

Awali, Ofisi ya Rais ilisambaza mwongozo kwa taasisi na mashirika ya umma unaoweka masharti ya ambayo watumishi wa umma wanaotaka kusafiri nje ya nchi watatakiwa kuyatimiza ili wapewe kibali cha kusafiri.

Masharti hayo ni kuomba kibali kwa Katibu Mkuu Kiongozi Sefue na maombi hayo yawasilishwe kwa Msajili wa Hazina kabla ya kwenda kwa Sefue ili mwombaji aweze kujenga hoja kwa kuzingatia umuhimu wa safari hiyo na tija itakayopatikana kutokana na safari hiyo.

Masharti hayo yanamtaka Mtendaji Mkuu wa Shirika ama taasisi apime aone kama safari hiyo ni muhimu  kuombewa kibali kwa Katibu Mkuu Kiongozi kabla ya kuwasilishwa Hazina.

Sharti lingine ni umuhimu wa safari hiyo na isipofanyika itaathiri vipi taifa na mwombaji  aeleze manufaa ya safari hiyo kwa taasisi na taifa kama imewahi kufanyika huko nyuma.


Ofisi za Umma zilipokea barua kutoka kwa Msajili wa Hazina Novemba 12 mwaka huu ikieleza kuwa Rais Magufuli ametoa zuio la jumla kwa safari za nje ya nchi katika utumishi wote wa umma na mihimili yake. Barua hiyo ya Hazina ilisema zuio hilo litadumu hadi pale itakavyoelekezwa vinginevyo.

No comments: