John Mnyika Apinga Tamisemi Kuhamishiwa Ofisi ya Rais - LEKULE

Breaking

14 Dec 2015

John Mnyika Apinga Tamisemi Kuhamishiwa Ofisi ya Rais



Mbunge wa jimbo la Kibamba, John Mnyika amekosoa uamuzi wa Rais John Magufuli wa kuhamishia wizara inayohusu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) chini ya ofisi yake, akidai kitendo hicho kimelenga kuvibana vyama vya upinzani ambavyo vimeshinda halmashauri nyingi nchini.
Mnyika (pichani) aliyasema hayo jana wakati akitoa shukrani zake kwa wananchi wa Kata ya Salanga iliyopo Kimara kwa kumchagua kuwa mbunge wao. Alieleza kushangazwa na mabadiliko yanayofanywa na Dk Magufuli tangu alipoingia madarakani.
Mbunge huyo alisema Chadema na vyama vingine vya upinzani vimeshinda katika uchaguzi wa nafasi za umeya na uenyekiti katika halmashauri mbalimbali nchini, jambo hilo limemfanya Rais kuiweka Tamisemi chini yake ili kupunguza uhuru wa halmashauri zinazoongozwa na upinzani katika kuleta maendeleo.
“Katika halmashauri za Dar es Salaam bado tunavutana, wanaleta madiwani wa viti maalumu kutoka Zanzibar kuja kupiga kura huku bara. Tunawaambia hatutakubali kwa sababu Chadema na Ukawa inaongoza kwa viti vingi vya udiwani, lazima tuongoze jiji hili,” alisema.
Mnyika aliongeza kuwa “Rais Magufuli amefanya kama alivyofanya Benjamini Mkapa wakati wa utawala wake kwa kutaka kutawala kibabe. Hatafika mbali kwa sababu ameshindwa kujenga mifumo thabiti, badala yake amebaki kuhimiza usafi wa siku moja,” alisema.

Kiongozi huyo ambaye pia ni naibu katibu mkuu wa Chadema, alimtaka Rais Magufuli kujenga misingi ambayo itajiendesha yenyewe bila uwepo wake. Alimtaka pia kuweka msimamo thabiti wa kutengeneza Katiba mpya kwa kufanyia kazi maoni ya wananchi.

No comments: