" Ewe Majaliwa Mwema, Hakikisha Unawatokomeza Panya Hao Wa Bandarini.." - LEKULE

Breaking

5 Dec 2015

" Ewe Majaliwa Mwema, Hakikisha Unawatokomeza Panya Hao Wa Bandarini.."

Ndugu yangu Majaliwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vinaonekana, vita unavyopigana kuwakomboa wanyonge walio wengi wa nchi hii.
Kazi unayoifanya hadi sasa inadhihirisha Rais wa Jamhuri, John Magufuli, hakukosea katika kulichagua ' tingatinga' la ukweli la kumsaidia kwenye kazi yake ya Urais.
Hapo bandarini yaonekana kuna mashimo mengi ya panya wanaotafuna mapato ya nchi. Na wengine ni mapanya buku mithili ya ukubwa wa sungura. Eti wanasema ' Bandari Kavu'. Kumbe, zimejaa mashimo ya panya. Iko wapi NASACO ya Watanzania? Miaka 54 ya Uhuru kwanini tushindwe kuendesha wenyewe bandari ya majini na nchi kavu badala ya kuwaachia panya wafanye kazi hiyo?
Ewe Majaliwa Mwema, vita ya panya wa bandarini kamwe isiwe na matokeo ya kutoka sare. Pambana na panya wezi na wenye kuficha mali zilizoibiwa na panya wezi wenzao.
Na ukitoka hapo bandarini na ushindi wa jumla, basi, utasonga mbele ukiwa na nguvu nyingi zaidi, na umma ulio nyuma yako, katika kumsaidia Rais wa Jamhuri kwenye vita ya pili ya ukombozi wa kiuchumi kwa nchi yetu tuliyozaliwa na tunayoipenda.

Wajumbe mnakaribishwa kuchangia...

No comments: