Nionavyo; Dr Shein Si Wa Kufanyiwa Uhuni Ule.. - LEKULE

Breaking

20 Nov 2015

Nionavyo; Dr Shein Si Wa Kufanyiwa Uhuni Ule..


Ndugu zangu,

Duniani hapa hakuna shule ya kujifunza uungwana. Watanzania leo tumeshuhudia jambo la aibu kubwa kwa taifa na mbele ya wageni kutoka nje wakiwamo mabalozi. Ni pale UKAWA walipoamua kumfanyia fujo Dr Ali Mohammed Shein, Rais wa Zanzibar alipokuwa akiingia Bungeni.
Kwangu tafsiri ya kwanza kwa kilichokuwa kikifanywa na UKAWA mle ukumbini ni wabunge wale wa UKAWA kukosa uongozi wenye kutanguliza hekima na busara. Mwenye kutanguliza hekima na busara, na kwa kuzingatia mila na desturi zetu za Kiafrika, jambo lile si la kuwaelekeza wafuasi wako kulifanya.
Na kilichoonekana pia ni ukweli kuwa ndani ya UKAWA ni wachache wenye nguvu hata za kuamrisha ambapo wengine hawawezi kupinga. Naamini si wote waliokuwa wakizomea walifurahia walichokuwa wakifanya, bali, walitaka kuwaonyesha waliowatuma kuwa wanafanya, maana, walionekana. Ni sasa, ndani ya UKAWA linaonekana pengo la viongozi wenye hekima na busara aina ya Dr Slaa na Profesa Lipumba.
Naamini kabisa, mbele ya Watanzania walio wengi, hakuna mavuno waliyoyapata UKAWA kwa kitendo kile walichomfanyia Dr Shein, bali hasara kubwa ya kisiasa. Kwa kitendo kile UKAWA wamejidhohofisha na wakati huo huo kuwaimarisha CCM.
Si ajabu, John Magufuli aliamua kushindilia msumari mwishoni mwa hotuba yake kwa kumwambia Spika awavumilie wapinzani na waendelee kuwafundisha. Akiwa na maana bado hawajakomaa.
Na kwa vile mtazamo huo wa Magufuli yumkini ndio unaofanana na wananchi wengi mitaani na vijijini, basi, hiyo ndio hasara ya kisiasa ninayoisema. UKAWA wana nafasi ya kujirekebisha, na waanze kwa kumwomba radhi Dr Shein na kuwaomba radhi Watanzania.

No comments: