Dr. Shein Aongozewa Muda Wa Urais Zanzibar - LEKULE

Breaking

2 Nov 2015

Dr. Shein Aongozewa Muda Wa Urais Zanzibar

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imetoa tamko kuwa Rais wa Zanzibar, Dkt. Ali Mohamed Shein, ataendelea kushikilia wadhifa huo hadi hapo rais mwingine atakapochaguliwa kihalali na kuapishwa.
 
Akitoa taarifa ya Serikali kwa vyombo vya habari mjini hapa jana, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais Mohamed Aboud Mohamed, alisema Katiba ya Zanzibar inamruhusu kuendelea na wadhifa huo hadi hapo atakapoapishwa Rais mwingine.

"Tunapenda kuwataarifu wananchi kwamba kwa mujibu wa kifungu cha 28 (1) (a) cha Katiba ya Zanzibar ya 1984 kinaweka sharti la kwamba mtu ataendelea kuwa Rais hadi Rais anayefuata ale kiapo cha kuwa Rais," alisema na kuongeza;

"Hivyo kwa kuzingatia maelekezo hayo ya Katiba, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inayoongozwa na Dkt. Ali Mohamed Shein, ipo na itaendelea kuwepo hadi hapo uchaguzi utakapokamilika na Rais atakayechaguliwa kula kiapo."

Mohamed alisema ni vizuri wananchi wakaelewa Rais wa Zanzibar anachaguliwa kwa mujibu wa kifungu cha 27 cha Katiba ya Zanzibar na sheria ya uchaguzi namba 11 ya 1984 ambayo imeweka utaratibu wa matokeo ya uchaguzi huo.

Sheria ya uchaguzi kifungu cha 42 (4) kinaeleza kuwa mgombea nafasi ya urais atatangazwa na Tume ya Uchaguzi Zanzibar baada ya kupata kura nyingi za halali.

Aidha, kifungu cha 42 (5) cha sheria ya uchaguzi kinakataza kwa mtu au taasisi yoyote kutangaza matokeo ya uchaguzi kinyume na sheria ya uchaguzi; na ni kosa la jinai kufanya hivyo."


"Serikali haitamvumilia mtu yeyote atakayekiuka sheria na atashughulikiwa kwa mujibu wa sheria. Na kwa taarifa hii, Serikali inaviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria kwa wale wote walioanza kufanya vitendo vya uvunjifu wa amani. Ni vizuri wananchi waendelee kuwa watulivu na kusikiliza taarifa za Serikali" alisema Aboud. 

No comments: