Polisi wasusia posho za kusimamia mitihani - LEKULE

Breaking

12 Sept 2015

Polisi wasusia posho za kusimamia mitihani

Askari wakiwa nje ya ofisi za Makao Makuu ya

Moshi. Polisi waliosimamia mtihani wa taifa wa kumaliza darasa la saba katika baadhi ya wilaya za mkoa Kilimanjaro wamekuja juu wakipinga kulipwa posho ya Sh22,500 kwa siku badala ya Sh40,000.
Wakati polisi waliosimamia mtihani huo katika mikoa mingine nchini wakilipwa posho ya Sh120,000 kwa siku tatu, polisi waliosimamia mitihani hiyo mkoani Kilimanjaro walilipwa Sh67,500 tu.
“Kiwango kipya cha posho kwa polisi kilichopitishwa mwaka huu ni Sh65,000 kwa siku tukasema hata kama wameshindwa kulipa kiwango hicho wangetulipa basi 40,000 kama wenzetu,” alidai mmoja wa polisi hao.
Polisi katika wilaya ya Hai, wao wameenda mbali na kususia malipo hayo na hadi jana mchana kulikuwa hakuna polisi aliyepokea malipo hayo ingawa walisimamia vyema mitihani hiyo.
Halmashauri pekee zinazodaiwa kulipa posho ya Sh40,000 kwa siku kama halmashauri nyingine nchini ni Same na Mwanga huku halmashauri nyingine zikidaiwa kulipa posho ya Sh22,500 kwa siku.
Kamanda wa Polisi mkoa Kilimanjaro, Fulgence Ngonyani alisema posho hizo zimelipwa kulingana na maelekezo ya Wizara na kwamba viwango vya posho viko tofauti kulingana na majukumu wanayokabidhiwa. “Wale waliosimamia vituo teule ambavyo ndivyo vinahifadhi mitihani na wale wanaosindikiza mitihani wao wanalipwa posho ya Sh40,00 kwa siku na wale wanaosimamia tu ni sh22,500 kwa siku,” alisema.

No comments: