Mbatia Amkaanga Dr. Slaa.......Ampa Makavu Samweli Sitta - LEKULE

Breaking

4 Sept 2015

Mbatia Amkaanga Dr. Slaa.......Ampa Makavu Samweli Sitta


MWENYEKITI Mwenza wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), James Mbatia, amewataka Watanzania kumpuuza aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa kwa kauli zake zilizojaa uchochezi na propaganda za siasa.

Pia alionya kauli za ovyo zinazotolewa na baadhi ya viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwamba wapinzani wakishinda vyombo vya ulinzi vitachukua nchi.

Alisema jeshi la Tanzania linasimamia misingi yake na kiongozi yeyote atakayeingia madarakani litafanya naye kazi kwa kuwa wote ni Watanzania.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana kufafanua mambo mbalimbali yalitamkwa  na Dk. Slaa juzi, Mbatia alisema  tuhuma alizozitoa kiongozi huyo zinalenga kuleta mpasuko katika taifa na kuvunja amani ya nchi.

Alisema hotuba nzima ya Dk. Slaa ililenga kumshambulia moja kwa moja Mgombea urais wa Ukawa, Edward Lowassa kwa sababu amekuwa tishio kwake na kwa CCM.

Mbatia ambaye pia ni Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, alisema mara zote propaganda kama hizo huwa zinafanywa na chama tawala ambacho kimekwisha kuona viashiria vya kuondolewa madarakani kupitia sanduku la kura.

Mbatia alitoa mfano kuwa kitendo cha Dk. Slaa kuwasingizia baadhi ya viongozi wa dini kwamba walihongwa na Lowassa ili wamuunge mkono ni hatua ya kuwataka waumini wasiwaamini viongozi wao jambo ambalo ni hatari kwa amani ya nchi.

“Hoja alizozitoa ni nyepesi ambazo Watanzania wanatakiwa kuzipuuza na wasikubali mpasuko hasa unaoletwa kwa mlengo wa imani ya dini.

“Kuwahusisha viongozi wa dini na tuhuma za uongo ni siasa nyepesi za mtaroni.

“Kusema eti Lowassa anaungwa mkono na Walutheri kwa sababu ni wenzake ni mpasuko mkubwa katika nchi,” alisema.

Mwenyekiti huyo wa NCCR Mageuzi alisema alisikitishwa na uongo uliosemwa na Dk. Slaa kwamba hakuunga mkono kuingia kwa Lowassa Chadema kwa sababu mwanasiasa huyo alishiriki kwa ukamilifu mchakato mzima wa kumshawishi Lowassa na wenzake kujiunga na Ukawa.

“Nimesikitishwa sana na uongo uliosemwa jana na kaka yangu Dk. Slaa kwa sababu  alishiriki katika kumshawishi Lowassa na wengine kujiunga nasi katika harakati za mabadiliko ya kweli,”alisema Mbatia.

Alisema kusema kwamba Lowassa alitoa ahadi ya kujiunga na Ukawa akiwa na kundi kubwa la wana CCM ni kutunga na hauna mashiko ya katiba na kanuni kwa vile  hakuna katiba yoyote ya chama cha siasa yenye masharti kama hayo.

“Lowasa alipokuja Ukawa hakutoa ahadi ya kuja na viongozi na pia hakuna masharti aliyopewa kwa sababu alifuata taratibu zote za kujiunga Chadema.

“Mbona mwaka 1995 yeye (Dk. Slaa) alipokatwa na CCM na kuhamia upinzani hakupewa masharti wala kubaguliwa?

“Katiba ndiyo inayotoa utaratibu wa mtu kujiunga na chama sasa yeye ni nani mpaka awe juu ya Katiba ya Chadema? Mbona yeye hakubaguliwa na aliendelea kufaidika hadi akagombea urais?” alihoji Mbatia.

Kuhusu kauli kwamba Dk. Slaa alikuwa hajaomba wala kuteuliwa na chama chake kugombea urais, Mbatia alisema kabla ya kuingia   Lowassa Ukawa, tayari Chadema kilikuwa kimekwisha kumteua Dk. Slaa kuwa mgombea ambaye angepambana na wenzake kutoka Chama Cha Wananchi (CUF) na NCCR.Mageuzi.

“Si kweli kwamba Dk . Slaa hakuwania nafasi ya kuteuliwa kugombea urais, bali chama chake kilikwisha kumteua na yalipojitokeza majina ya Profesa Ibrahim Lipumba na Dk. George Kahangwa, alisema yeye ndiye mwenye vigezo vyote vya kuteuliwa kuwa mgombea wa umoja huu.

“Tulifanya vikao mbalimbali kikiwamo tulichofanya nyumbani kwa Profesa Lipumba lakini hatukufikia muafaka, lakini baada ya Lowassa kujiunga tulimwomba kwa pamoja agombee urais.

“Sababu iliyotufanya tumshawishi Lowassa agombee nafasi hiyo ni nyota yake ya siasa aliyonayo. Je, haya mafuriko tunayoyapata na tuliyopata pale Jangwani tungeyapata?

“Hizo tuhuma za ufisadi wanazozitoa juu ya Lowassa …tukianza kuwataja kwa masakata yaliyotokea katika uongozi wa Rais Kikwete (Jakaya) hakuna hata mtu mmoja atakayebaki.

“Sakata la EPA, BoT (Benki Kuu), Deep green, Richmond, vichwa hewa vya treni… hakuna atakayebaki msafi. Hivyo ufisadi si mtu bali mfumo,” alisema Mbatia.

Alisema mgombea urais wa CCM, Dk. John Magufuli, anaweza kueleza namna alivyosimamia uuzwaji wa nyumba za serikali.  Je, huo siyo ufisadi?

Mbatia alisema   wale wanaotaka mdahalo na Lowassa si saizi yake bali yeye ndiye anaweza kupambana nao.


Alimtaka Waziri wa Uchukuzi, Samueli Sitta, kuwaeleza Watanzania fedha za serikali alizotumia kujengea nyumba ya Spika kule Ulambo wakati akijua usipika ni kazi ya muda tu.

No comments: