Maalim Seif kumaliza matatizo ya maji na umeme pindipo akichaguliwa kuwa Rais - LEKULE

Breaking

13 Sept 2015

Maalim Seif kumaliza matatizo ya maji na umeme pindipo akichaguliwa kuwa Rais



Katibu Mkuu wa CUF Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akizungumza na vijana wa barza mbali mbali katika jimbo la Mfenesini.(Picha na Salmin Said, OMKR).




Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi CUF Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, amesema anakusudia kumaliza matatizo ya maji na umeme katika visiwa vya Unguja na Pemba iwapo wananchi wa Zanzibar watamchagua kuwa Rais katika uchaguzi mkuu ujao.

Amedai kuwa Serikali inayoongozwa na Chama Cha Mapinduzi imeshindwa kumaliza matatizo hayo kwa kipindi cha miaka 53, hivyo wakati umefika wa kufanya mabadiliko ya kiuongozi ili kumaliza matatizo hayo.

Akiwa katika ziara ya kutembelea matawi na barza za Chama hicho Jimbo la Mfenesini, Maalim Seif amesema katika kumaliza changamoto hizo hatowabagua wananchi kwa misingi yoyote ikiwemo ya kidini, kabila, siasa au eneo mtu analotoka.


Amesema huu ni uchaguzi wa kufanya maamuzi juu ya hatma ya Zanzibar na mamlaka yake, na kwamba chama chake ndicho chenye dhamira ya kuongoza mabadiliko kwa kuzingatia maslahi mapana ya Wazanzibari.

Amewakumbusha masheha kutekeleza majukumu yao bila 
kuingiza utashi wa kisiasa, kwa kuzingatia kuwa wao ni watumishi wa serikali na kamwe hawatakiwa kuwa wanasiasa.

Amesema wananchi wana haki ya kikatiba ya kujiunga na vyama wanavyotaka, hivyo amewataka kutoogopa kutekeleza wajibu huo.

Amefahamisha kuwa dhamira ya CUF ni kuwaunganisha wazanzibari sambamba na kuleta mabadiliko ya kweli, ili wananchi watumie uhuru wao kikamilifu bila kunyanyaswa.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar Mhe. Nassor Ahmed Mazrui amewataka wananchi kuungana na kuendelea na mshikamano wao, ili kuhakikisha kuwa wanakipatia ushindi chama hicho.

Miongoni mwa maeneo aliyoyatembelea ni pamoja na Mashimo ya  mchanga shehia ya Kihinani, barza ya CUF meli nane, Bumbwisudi na Mfenesini.

No comments: