Hofu yatanda, silaha za kivita kukamatwa - LEKULE

Breaking

8 Sept 2015

Hofu yatanda, silaha za kivita kukamatwa


SILAHA (1)-001Silaha zilizokamatwa zikioneshwa kwa wandishi wa habari.
Na Timu ya Uwazi, Mkuranga
HOFU kubwa imetanda kwenye Kijiji cha Mamndi Mkongo kilichopo Wilaya ya Mkuranga, mkoani Pwani kufuatia Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam kwa  kushirikiana na wale wa mkoa huo kunasa silaha  nyingine za kivita zikiwa zimefukiwa kwenye shimo msituni.
Tukio hilo  la unasaji wa silaha lilifanikiwa Agosti 29,  mwaka huu  katika msitu  mmoja uliopo  katika kijiji hicho  kilichopo umbali wa kilomita 23  kutoka mjini Mkuranga.
NI KAWAIDA YA UWAZI
Baada ya Uwazi kuzipata taarifa za polisi kuzinasa silaha hizo lilifunga safari hadi kwenye eneo la tukio na kushuhudia shimo ambalo silaha hizo za kivita zilifukiwa kwa utunzaji wa siri.
SILAHA (6)-001Silaha za kigaidi zilizokamatwa.
MKUU WA MGAMBO ASIMULIA
Katika Mahojiano maalum na kiongozi wa wanamgambo wa  Kata  ya Bup iliyopo kwenye kijiji hicho, Mussa Mohammed Koti alisema wamekuwa  wakifanya doria  katika mazingira magumu na hasa baada  ya vikosi  vilivyokuwepo kuondoka. Awali huku kulikuwa na vikosi maalum vya ulinzi na usalama.
SILAHA (7)-001Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova akizungumza na wandishi wa habari.
SIKU SILAHA ZILIPOKAMATWA
Koti alisema  hata  silaha  hizo  za  kivita  zilizokamatwa  Agosti 29, mwaka huu zilikuwa  juhudi za wanamgambo wake, polisi  walikuja  kujulishwa baadaye.
“Siku hiyo nakumbuka, ilikuwa mchana. Wanamgambo waliingia msituni kwa lengo la kufanya doria. Wakafika sehemu na kukuta mti umepandwa kwa kupinduka, juu chini, chini juu.
“Mmoja wao akashtuka na kuwaambia wenzake kwamba, pale pana tatizo. Akasimama eneo lile na kupiga mguu chini, ukatoka mlio kama sehemu yenye shimo kwa chini. Tulipanga kufukua ili kujua ndani yake mna nini!”
HOFU (1)-001Moja kati ya mahandaki zilimokuwa zimefukiwa silaha hizo.
HOFU (3)-001
Ngome ya magaidi hao iliyoteketezwa na Jeshi la Polisi.

POLISI WAJULISHWA, WATOA KIBALI
“Lakini kwanza tulifanya mawasiliano na Jehi la Polisi Mkuranga na kuwaelezea tunachotaka kukifanya, wao wakatupa kibali cha maneno cha kufukua, maana tuliwapigia simu. Ndipo tulipozikuta silaha hizo.”

HOFU (4)-001
WAIJARIBU SILAHA MOJA
“Silaha hizo zilikuwa zimechakaa kidogo kiasi kwamba tulihisi hazifanyi kazi. Tukawapigia tena polisi, wakasema tuijaribu bunduki moja ili kuona kama itafanya kazi au la!
“Kwa sababu wanamgambo wangu wamepitia mafunzo ya kijeshi, mmoja alifyatua bunduki akiielekeza hewani ambapo risasi moja ilitoka. Tukaamini zote ziko vizuri, tukawajulisha polisi ambapo walifika na kuzichukua.”
HOFU (5)-001SILAHA ZILIZOKUTWA
Uwazi lilizungumza na kamati ya ulinzi na usalama kijijini hapo na kusema silaha zilizokutwa ni bunduki za kivita aina ya AKA 47 (moja), SRA  (mbili), RPG (mbili) Greana (moja) na risasi 388, tambi za milipuko mikali, kitabu cha muongozo wa kijeshi, kemikali za kutengeneza mabomu ya kutupa kwa mkono na kitabu chenye maelekezo ya namna ya kujibadili kuwa mwanamke au mwanaume.
HOFU (6)-001MTU HUYU ANATUHUMIWAJE?
Koti alizidi kueleza kuwa, katika hali ya kushangaza, mwanakijiji mmoja (jina linahifadhiwa kwa sasa), ambaye wakati wa zoezi la ufukuaji hakuwepo, alirudi baada ya polisi kufika na kuondoka na silaha hizo, akiwa na bodaboda mbili. Moja iliendeshwa na mtu ambaye si mwenyeji kwenye macho ya wanakijiji hao akiwa amejiziba sehemu kubwa ya uso wake.
HOFU (2)-001Wawili hao walisimamisha pikipiki nje ya nyumba ya udongo ya mwenyeji huyo na kuchukua familia yake yenye mke na watoto. Kisha wakapanda kwa mtindo wa ‘mishikaki.’
“Sasa wakati wanaondoka, wanakijiji waliwafuata lakini yule mwenyeji akasema anayejiona ni mwanaume kweli awafuate jambo lililowafanya wanakijiji hao kusita.
“Ndipo wakaenda kuchoma moto nyumba yake. Lakini ndani ya nyumba ile kulikutwa kofia aina ya kapelo ambayo ina alama ya sime mbele. Pia kulikutwa magaloni ambayo yanasadikiwa kubebea kemikali za kutengenezea milipuko.”
HOFU YA WANAKIJIJI
Koti aliendelea kusema kuwa, anaiomba serikali kuwawekea ulinzi wanakijiji wake kwa kuwa licha ya wengine kukamatwa, washukiwa hao waliotoroka wanaweza kurudi kinyemela kijijini hapo na kuwafanyia ugaidi kama njia ya kulipa kisasi baada ya shimo lao lenye silaha kugunduliwa.
Miongoni mwa mambo waliyoomba wanakijiji hao ni kupatiwa silaha na pikipiki zitakazotumika na wanamgambo wao katika kufanyia doria.
TUJIKUMBUSHE
Kwa mujibu wa chanzo chetu, awali baada ya jeshi la polisi kunyetishiwa kuhusu uwepo wa silaha na magaidi kwenye Wilaya ya Mkuranga, Kikosi  Maalum cha Ulinzi na Usalama (task force)  kiliweka kambi  katika kata hiyo kwa  ajili ya kuwawinda wahalifu wanaofanya matukio mbalimbali mijini kisha kukimbilia katika misitu hiyo kama makazi yao ya kujificha.
Uwekaji wa kambi wa kikosi hicho kulizaa matunda  ambapo wahalifu kadhaa walikamatwa kutokana na matukio mbalimbali ya vitendo  vinavyoashiria ugaidi.
Mbali na hilo, pia kikosi hicho kilifanikiwa kufukua begi  lililokuwa na kiasi cha shilingi milioni mia moja na hamsini (150,000,000) kitu ambacho mmoja wa wanakijiji hicho alisema huenda pesa hizo ziliandaliwa kwa ajili ya kufanyia mafunzo maalum ya kijeshi kwa vijana ambao wangewakusanya ili kufanikisha adhima yao ya ugaidi.
KAMANDA KOVA AONGEA NA UWAZI
Hivi karibuni, Kamishna wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alitangaza kufukuliwa kwa silaha zingine za kivita katika msitu huo uliopo kijijini hapo.
Kamishana Kova mbali na kutangaza mafanikio ya ukamataji wa silaha hizo, pia alisema jeshi hilo limefanikiwa kuwatia mabaroni watu 38 wanaotuhumiwa kwa ugaidi na mahojiano yanaendelea kwa kasi kubwa.
“Mpaka sasa tunawashikilia watu 38  lakini sitataja majina yao kwa sababau za kiupelelezi, muda  ukifika tutaweka wazi majina na hata picha zao,” alisema Kamanda Kova.
Imeandaliwa na Haruni Sanchawa na Richard Bukos.

No comments: