CCM; HUU SI WAKATI WA KUMSEMA LOWASSA NI WA MABADILIKO - LEKULE

Breaking

8 Sept 2015

CCM; HUU SI WAKATI WA KUMSEMA LOWASSA NI WA MABADILIKO

RAIS wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kuwaambia wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa, wananchi wanataka mabadiliko, akasema wasipoyapata ndani ya CCM watayatafuta nje ya CCM.
Maneno haya ya Mwalimu ni nguzo ya CCM, kwamba uhai wa chama hicho hautatokana tena na ukongwe wake bali mfumo wa mabadiliko ambao rais wa kwanza aliuona kuwa ndiyo kiu ya wananchi wengi hivi sasa.
lowassa2.jpgKiu ya mabadiliko aliyoiona kiongozi huyo wa zamani wa CCM ilikwenda mbali zaidi kiasi cha kuwafanya wananchi wawe tayari kukihama chama kilichowalea kwa miaka nenda rudi na kujitafutia mabadiliko nje ya chama hicho kikongwe.
Nilitaraji viongozi wa chama hicho hasa katika kipindi hiki cha uchaguzi wangetambua maono ya Nyerere na kuyaishi kwa lengo la kukinusuru chama kisianguke.
Pengine msemo wa wahenga una maana; kwamba sikio la kufa halisikii dawa ndiyo maana CCM inapuuza wosia huo wa mabadiliko na sasa kinajikita katika siasa za kushambulia watu kwa kutumia mbinu mbalimbali.
Nashibisha hoja; akiwa kwenye moja ya kampeni zake za urais mgombea wa vyama vinavyoundwa na Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward Lowassa hivi karibuni mkoani Tabora alipokelewa na mabango mbalimbali lakini moja lililokuwa na maana kwangu lilisomeka hivi:
“Lowassa angekuwa shetani, Magufuli (John, mgombea wa CCM) angekuwa Mungu tungemchagua shetani kwani tumeichoka CCM.” Ni maneno machache lakini yana maana kubwa. Kwamba wananchi wako tayari kumbadili Mungu kwa shetani.
Hoja ni ‘wananchi kutaka mabadiliko’ siyo kitu kingine. Siyo ushetani wa mgombea fulani wa chama fulani, watu wako tayari kukata kiu yao ya mabadiliko mahali popote, amshaamsha ya upinzani inachochewa na kiu ya mabadiliko, si kitu kingine.
Hoja za mgombea urais wa Ukawa kuwa fisadi, mgonjwa, siyo msafi, amekumbatia mtandao wa wezi zinaeleweka kama bango la wananchi wa Tabora lilivyosomeka kwamba wao wako tayari kumchagua shetani ili tu wapate mabadiliko.
Katika hili CCM wanashindwa nini kubadili gia angani, wanakwazwa na kipi mpaka wasiwapatie wananchi mabadiliko wayatakayo? Kuna ugumu gani wa kuwaaminisha wananchi kuwa chama kitakachokata kiu ya mabadiliko ni CCM?
Ahadi: CCM iko tayari kujisahihisha yenyewe kwanza. Serikali yake italeta mabadiliko ya mfumo wa afya, elimu, utumishi, utoaji haki, usimamizi wa rasilimali za nchi na mabadiliko makubwa katika uendeshaji wa serikali kwa ujumla wake kwa lengo la kuwatoa wananchi kwenye hali ya umaskini. CCM ikijinadi hivi haitashangiliwa kweli?
Naweza kuulizwa na CCM; tumekuomba ushauri? Hakika nitasema la! Lakini uungwana ni vitendo. Naandika haya kukisaidia mawazo chama hiki kikongwe kijitambue ili kijiweke kwenye misingi mizuri ya kushindana katika uchaguzi huu na kupata ushindi wa haki ambao utalinusuru taifa hili na vurugu.
Niwaambie wanaoendesha kampeni za majukwaani wakitaka kushawishi umma hawana budi kurudi kwenye msingi wa mabadiliko. Wamnadi mgombea wao kuwa ni mtu atakayeweza kuwasaidia wananchi kupata wanachokihitaji, waache kumshambulia mtu ambaye wamekuwa naye kwenye uongozi miaka nenda rudi akiwa msafi au mchafu.

Kwangu mimi huu si wakati wa CCM kumsema Lowassa, ni wakati wa kueneza sera za mabadiliko yatakayolitoa taifa hili kutoka hapa tulipo kwenda mahali pengine pazuri zaidi. Mambo ya ufisadi tuviachie vyombo vya usalama vishughulike na watuhumiwa. Kumsakama mtu majukwaani ni kumtafutia huruma kwa wananchi.

No comments: