Balozi Seif Ajumuika na Wanamichezo wa Jimbo la Konde Pemba - LEKULE

Breaking

17 Sept 2015

Balozi Seif Ajumuika na Wanamichezo wa Jimbo la Konde Pemba

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akishiriki kwenye matembezi yaliyotayarishwa na Vikundi vya Mazoezi vya Jimbo la Konde hapa katika Kijiji cha Msuka, Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba.kulia ya Balozi Seif ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kaskazini Pemba Mzee Mberwa Hamad Mberwa na Mkuu wa Mkoa huo Omar Khamis Othman.
Baadhi ya wanamichezo wa vikundi vya mazoezi wa Jimbo la Konde na wale waalikwa wa Wilaya ya Wete na Chake chake wakishiriki kwenye matembezi ya kuimarisha vikundi hivyo yaliyoongozwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif.
Wanamichezo wa vikundi vya mazoezi wakifanya vitu vyao       { Mchaka mchaka na mazoezi ya viungo } baada ya kumaliza matembezi yao yaliyoongozwa na Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akizungumza na wanamichezo mbali mbali walioshiriki matembezi na mazoezi ya viungo huko katika Kijiji cha Msuka Jimbo la Konde Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba.



Wanamichezo Nchini ambao ndio kundi kubwa  katika Jamii wamekumbushwa wajibu wao wa kushiriki vyema katika kuimarisha  suala la Amani ili kulifanya Taifa kuendelea kuwa Kisiwa cha Amani Duniani hasa ikizingatiwa kwamba  liko  katika kipindi cha mpito kuelekea uchaguzi Mkuu wa Mwezi Oktoba mwaka huu.

Kumbusho hilo limetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipokuwa akizungumza na Wanamichezo tofauti waliounda Kundi la Mazoezi Jimbo la Konde baada ya kushiriki nao matembezi yaliyoambatana na mazoezi na kuishia katika uwanja wa Michezo wa Okapi katika Kijiji cha Misuka Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Balozi Seif Ali Iddi alisema kwa vile uimarishaji wa Suala la Amani unamgusa kila mwana Jamii juhudi za ziada zinastahiki kuchukuiliwa ili  kuwawezesha Wananchi waendelee  kufanya shughuli zao za kawaida za kila siku ikiwemo michezo.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na ile ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania zitahakikisha kwamba Amani ya Taifa inadumu na Wananchi wote wanaendelea kuwa washirika wa Amani hiyo.

Alitahadharisha kwamba tabia ya baadhi ya Watu kujaribu kuichezea amani iliyopo kwa kujaribu kuiga mifano ya Mataifa mengine hasa yale ya jirani ni kujenga misingi mibaya ya kusababisha migogoro itakayozua balaa na migogoro isiyokwisha.




“ Tusipendelee kabisa kutaka kuiga wenzetu wa Mataifa jirani katika kujaribu kuichezea amani ambayo tumekuwa wakati wote tukishuhudia Watoto na Akina Mama wa Mataifa hayo wanavyopata madhila ikiwemo kudhalilishwa Kijinsia baada baadhi yao kuichezea ”. Alisema Balozi Seif.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar amewataka wananchi wote Nchi kujenga utamaduni wa kushiriki kwenye mazoezi kwa kujiunga na Vikundi tofauti ili kujenga afya zao sambamba na kuimarisha Umoja na Mshikamano miongoni mwao bila ya kujali itikadi na jinsia zao.

Alisema mazoezi pekee yanatosha kuwa tiba kwa kuondoa maradhi madogo madogo na pia yanasaidia kuchangia kwa asilimia kubwa akili Timamu kwa mtu anayeshiriki mazoezi kila siku.

Katika kuunga mkono vikundi hivyo vya mazoezi Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliahidi kusaidia seti za Jezi na Mipira kwa Timu za Mpira wa Kandanda na zile za Pete zilizomo kwenye kundi hilo la Mazoezi.

Balozi Seif alifahamisha kwamba Serikali Kuu kupitia Wizara inayohusika na shughuli za Michezo itaangalia njia mbadala zitakazosaidia kutatua baadhi ya changamoto zinazowakabili wanamichezo hao ikiwemo mashine za kupimia afya na sare za mazoezi.

Aliwapongeza Wanamichezo hao wa Konde kwa uamuzi wao wa kubuni wazo la kuanzisha vikundi vya mazoezi ambavyo mbali ya kujenga afya lakini pia kwa kiasi kikubwa vinasaidia kuimarisha Umoja na Mshikamano miongoni mwao bila ya kujali tofauti zao za Kisiasa.

Akisoma Risala ya Wanamichezo hao wa Vikundi vya Mazoezi wa Jimbo la Konde Laila Ali Omar alisema vikundi hivyo vilivyojumuisha michezo tofauti vimeamua kuendeleza michezo ili kuimarisha sanaa kama agizo la Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo linavyoelekeza.

Laila alisema Wizara  inayosimamia Michezo imekuwa ikiwasisitiza wana Jamii hasa Vijana kushiriki michezo kwa nia ya kujenga afya, kuimarisha umoja, mshikamano unaojumuisha zaidi Vijana ili wajiepushe na vikundi vinavyoweza kuwashawishi kujiingiza katika matendo maovu.

Alieleza kwamba licha ya mafanikio makubwa yaliyopatikana tokea kuasisiwa kwa vikundi hivyo likiwemo sauala la  umoja lakini bado kundi hilo kubwa linakabiliwa na changamoto zinazosababisha kudumaza kwa malengo waliyoyakusudia.

Laila alizitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na wanamichezo hao kukosa sare na jezi za mazoezi na kuiomba Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Zanzibar kuwa karibu na vikundi hivyo kwa lengo la kuvipatia huduma na ushauri.

Akimkaribisha mgeni rasmi katika hafla hiyo Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo Zanzibar Bihindi Hamad alisema Wizara hiyo wakati wote inaendelea kushirikiana na wanamichezo wote katika kuhakikisha kwamba Sekta ya michezo  inaimarika zaidi.

Bihindi alisema muendelezo wa Vikundi vya Michezo hasa vile vya mazoezi ni jumla ya jitihada za Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezi katika kuwashajiisha Vijana  Nchini kushiriki kwenye michezo kwa lengo la kuenga afya na kupunguza Maradhi.

No comments: