NEC Yawatoa Hofu Watanzania......Yasema Hakuna Wizi wala Uchakachuaji wa Kura Mwaka huu - LEKULE

Breaking

17 Aug 2015

NEC Yawatoa Hofu Watanzania......Yasema Hakuna Wizi wala Uchakachuaji wa Kura Mwaka huu



Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), imesema kuwa imeunda timu ya ushindi ya kuhakikisha matokeo ya uchaguzi mkuu wa Oktoba, mwaka huu yanatangazwa kwa wakati, ya kweli na haki kwa pande zote.

Akizungumza na gazeti  la Nipashe jana lililotaka kujua mipango ya Tume ili kuondoa malalamiko ya wananchi, vyama vya siasa, wagombea na wadau kuhusu kucheleweshwa matokeo na kuzua hofu ya uchakachuaji, Mkurugenzi wa Nec, Ramadhani Kailima, alisema timu hiyo itakuwa na wajibu mkubwa na hakuna kulala hadi matokeo yote yawe wazi.

“Tutakuwa na timu ya ushindi kutangaza matokeo yote mapema, hakuna kulala hadi tutoe matokeo kwa wakati, ya haki na kweli na yanayoaminika kwa wapigakura,” alisema.

Alisema malalamiko ya kupendelewa kwa chama chochote hayana msingi wowote kwa kuwa Tume haina chama na haitapendelea chama zaidi ya kuweka wazi matokeo yote itakayoyapata kwa wakati kwa kuwa watakuwa wanafanya kazi kisasa zaidi.

Alipoulizwa juu ya uzoefu wa Tume miaka ya nyuma kuhusiana na kuchelewesha matokeo hata ya maeneo ya mijini kunakofikika kirahisi, Kailima alisema kama kutakuwa na ucheleweshaji sababu zitawekwa wazi na wapigakura watatangaziwa bila kificho.

“Ya 2010, yasizungumziwe sasa kwa kuwa tunafanya kazi kisasa kuhakikisha matokeo yanakuwa wazi na kila hatua wananchi watatangaziwa,” alisema na kuongeza:

“Tunawaomba wananchi mara baada ya kupiga kura wakae mbali na ikiwezekana waende nyumbani kwa kuwa kila kituo cha kupigia kura kutakuwa na mawakala kama kuna tatizo lolote la kufanya matokeo yasitangazwe kwa wakati, watajulishwa mapema.”

Kailima alisema Nec iko huru na inatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa sheria na kanuni na haiingiliwi kokote kwani katika kugawa majimbo, Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho kinadaiwa kubebwa na Tume, kimelalamika na kama wangekuwa wanapendelewa, ni wazi kuwa malalamiko yao yangesikilizwa, lakini Tume imeamua kufanya kazi zake kwa uhuru.

“Uhuru wetu siyo jina, bali ni kutekeleza majukumu ya kikatiba na sheria bila kuingiliwa, kiwe chama au mtu hawaruhusiwi kutangaza matokeo ya uchaguzi, bali msimamizi wa uchaguzi wa kata atatangaza ya kata, ubunge yatatangazwa na Mkurugenzi wa Manispaa, mji au halmashauri na Tume itatangaza matokeo ya urais,” alisema.

Alisema watumishi wote wa Tume kabla ya kufanya kazi huapishwa kujiondoa au kukana itikadi ya chama chake na kuanza kutekeleza majukumu yake ili kusiwe na upendeleo kutokana na itikadi.

Alipoulizwa kuhusu matukio kadhaa yaliyotokea katika uchanguzi mkuu wa mwaka 2010 ikiwamo wasimamizi wa baadhi ya majimbo mfano, Shinyanga mjini kutoroka baada ya kutangaza matokeo yenye utata yaliyompa ushindi mgombea wa CCM na kuzua vurugu, Kailima alisema:

“Tuko 2015, tumejipanga kikamilifu, ndiyo maana tuna timu ya ushindi kuhakikisha hakuna ucheleweshwaji wa matokeo. Itakuwa Tume tofauti na ya miaka mingine.”

No comments: