Mnyika Asema Kampeni za UKAWA Zitazinduliwa na Dr. Slaa - LEKULE

Breaking

10 Aug 2015

Mnyika Asema Kampeni za UKAWA Zitazinduliwa na Dr. Slaa


Baada kimya cha muda mrefu hatimaye Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Wilibrod Slaa, anatarajiwa kufungua pazia la kampeni za Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

Imeelezwa kuwa, Dk. Slaa ambaye kwa sasa amepewa likizo na chama chake baada ya Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, kujiunga na chama hicho, atafungua kampeni za Ukawa mkoani Dar es Salaam mwezi huu.

Kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka huu zitaanza rasmi Agosti 22, mwaka huu.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Naibu Katibu Mkuu Bara wa Chadema, John Mnyika, alidokeza kwamba Dk. Slaa atazindua kampeni za Ukawa katika Jimbo la Kibamba, ambalo yeye (Mnyika) anagombea ubunge kwa tiketi ya umoja huo.

Mnyika alidokeza hayo mwishoni mwa wiki alipozungumza na viongozi wa matawi na kata ya Goba, muda mfupi kabla ya kufanyika uchaguzi wa kura za maoni kumchagua mgombea udiwani katika eneo hilo.

“Dk. Slaa yupo mapumzikoni na jana nilizungumza naye kwa kirefu na aliniambia bado anapumzika, lakini atakuja kushiriki kampeni Jimbo la Kibamba ambalo mimi nagombea ubunge,” alisema Mnyika.

Hata hivyo, Mnyika alipoulizwa kama Dk. Slaa atashiriki kampeni za nchi nzima ama ataishia Jimbo la Kibamba pekee kama alivyozungumza naye, Mnyika hakutaka kufafanua zaidi.

Katibu huyo wa Chadema hajashiriki katika shughuli mbalimbali za Ukawa ikiwamo kikao cha Ukawa cha kumkaribisha Lowassa kwenye makao makuu ya Chama cha Wananchi (Cuf), mapokezi ya mwanasiasa huyo na mkutano mkuu wa Chadema uliompitisha kugombea urais kupitia Ukawa.

Hata jana Dk. Slaa hakuhudhuria mkutano wa Baraza Kuu la Taifa la Cuf ambao ulihudhuriwa na viongozi wote wakuu wa vyama vinavyounda Ukawa vya Chadema, Cuf, NCCR-Mageuzi na NLD.

Waliohudhuria jana ni Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe; Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia na Mwenyekiti wa NLD, Dk. Emmanuel Makaidi.

Pia walikuwapo wagombea urais wa Jamhuri ya Muungano, Edward Lowassa na Katibu Mkuu wa Cuf, Maalim Seif Sharif Hamad na mgombea mwenza, Juma Haji Duni.

Akizungumza katika mkutano mkuu wa Chadema wiki iliyopita, alinukuliwa na vyombo vya habari akisema kuwa, Dk. Slaa kwa sasa yupo mapumzikoni, lakini kampeni zitakapoanza ataongoza kampeni za Ukawa  kuhakikisha wanaibuka na ushindi kwa ngazi ya udiwani, ubunge na urais.

Mnyika aliwaeleza wananchi wa kata hiyo kuwa Ukawa utashinda uchaguzi huu na kwamba kinachotakiwa ni wao kujiandaa kufanya kampeni za nguvu ili kuwafikia wananchi wengi.

Hata hivyo, Dk. Slaa alipotafutwa jana kuthibitisha maelezo ya Mnyika, simu yake ya mkononi haikupatikana.
 
Hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa maandishi (sms) hakujibu.

Habari za Dk. Slaa kuzindua kampeni za Ukawa kama zitakuwa ni za kweli itakuwa faraja kwa wafuasi na viongozi wa vyama vinavyounda Ukawa.

Katika hatua nyingine, Chadema imeelezea hofu ya kuwapo kwa waraka wenye maagizo kwa vyombo vya dola ukitaka  wakusanye vitambulisho vyao vya kupigia kura kwa lengo linalohusishwa na hujuma za uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 25, 2015.

Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika juzi eneo la Kimara Matangini jijini Dar es Salaam, Mnyika alisema wamepata taarifa kutoka kwenye chanzo chao kuwa askari na maOfisa wengine wa vyombo vya dola, wamepewa maagizo na wakubwa wao kukusanya vitambulisho vyao vya kupigia kura ili namba zao zisajiliwe.

Alisema Rais Jakaya Kikwete, kwa nafasi yake kama Amiri Jeshi Mkuu, anatakiwa kuingilia kati suala hilo na pia kuitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kujitokeza kukemea suala hilo.


Hata hivyo, Msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Bulimba, alipoulizwa alisema habari hizo ni za uzushi na kwamba hakuna maagizo kama hayo.

No comments: