Majeruhi wa bodaboda wajaza wodi Muhimbili - LEKULE

Breaking

27 Aug 2015

Majeruhi wa bodaboda wajaza wodi Muhimbili


Dar es Salaam.
Kuongezeka kwa majeruhi wa ajali za bodaboda kumeifanya Taasisi ya Mifupa Muhimbili (Moi), kuzidiwa na wagonjwa hadi kulazimika kuwalaza wengine sakafuni.

Ofisa Uhusiano wa Moi, Patrick Mvungi alisema asilimia 53 ya majeruhi wote wanaopokewa na taasisi hiyo ni wa ajali za pikipiki.
Wajumbe wa Kamati ya Usalama Barabarani, Kanda ya Dar es Salaam jana walitembelea wodi namba 17 na 18 za Jengo la Sewahaji na Wodi namba Mbili ya Jengo la Mwaisela na kujionea idadi kubwa ya majeruhi. Majeruhi wengi waliolazwa Sewahaji ni vijana ambao baadhi yao wamekatika miguu, mikono na wengine wakiwa na majeraha vichwani.
Mvungi alisema kila siku taasisi hiyo inapokea majeruhi kati ya 20 na 26 na kwamba wengi wao ni wa ajali za pikipiki. “Wodi za kulaza majeruhi zimezidiwa tunalazimika wengine kuwalaza chini lakini wote wanapata matibabu,” alisema.
Alisema Wodi Namba Mbili, ambayo ni ya majeruhi wanawake, ina vitanda 33 lakini hadi jana ilikuwa na wagonjwa 54 na kwamba waliozidi wanalala sakafuni.
Alisema tatizo la wagonjwa kulala sakafuni liko katika wodi tatu zinazolaza majeruhi... “Tatizo hilo litamalizika hivi karibuni mara baada ya kumalizika kwa jengo la taasisi.” Katika wodi ya wanaume namba 17 na 18 ya Jengo la Sewahaji, mmoja wa majeruhi hao, Fikiri Omari (31) aliyevunjika mguu wa kulia, alisema alipata ajali ya pikipiki tangu Juni 28 na kwamba mipango yake imeharibika.
Alisimulia kwamba alipata na mkasa huo wakati akisubiri kuruhusiwa kwenye taa za barabarani baada ya kugongwa na gari ambalo halikusimama.
“Nina mke na watoto wanaonitegemea lakini miezi inazidi kupita nikiwa hospitalini huku hali yangu ikiwa bado mbaya,” alisema. Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama Barabarani Kanda ya Dar es Salaam, Fadhili Mgonja alisema: “Ninasikitika kuwaona vijana wadogo wakiwa wamekatwa viungo kwa sababu ya ajali za barabarani.”
Alisema madereva, hasa wa bodaboda, wanatakiwa kuwa makini wanapokuwa barabarani kwa sababu wengi wao hawafuati sheria. “Madereva wa bodaboda hawafuati sheria na hata askari wa usalama barabarani wakiwasimamisha hawasimami matokeo yake ni ajali,” alisema.

No comments: