Magufuli Kuishika Dar Leo Wakati Akizindua Kampeni - LEKULE

Breaking

23 Aug 2015

Magufuli Kuishika Dar Leo Wakati Akizindua Kampeni


CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kinatarajiwa kuzindua kampeni zake za urais, ubunge na udiwani nchi nzima katika viwanja vya Jangwani leo, katika mkutano utakaorushwa moja kwa moja na televisheni na redio mbalimbali nchi nzima.

Katika uzinduzi huo, CCM pia inatarajiwa kuweka ilani yake ya uchaguzi hadharani, itakayonadiwa na mgombea urais wake, Dk John Magufuli na wagombea wengine wa ubunge na udiwani nchi nzima.
 
 Moja ya mambo ambayo CCM inatarajiwa kufafanua ni matumaini makubwa ya uwezo wa mgombea wake katika kusimamia utekelezaji wa ilani hiyo, kutokana na historia yake ya utendaji ndani ya Serikali katika nafasi mbalimbali alizokabidhiwa, ikiwemo Waziri wa Ujenzi.

Wageni mbalimbali pia wamealikwa kuhudhuria uzinduzi huo vikiwemo pia vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
 
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Msemaji wa CCM Mkoa, Juma Simba alisema vile vile wanatarajia wageni kutoka ndani na nje ya jiji la Dar es Salaam kuhudhuria mkutano huo leo. 
 
“Tumetuma mialiko ya mkutano wa kesho (leo) sio tu kwa wana CCM wenzetu bali pia kwa vyama vingine vya siasa ikiwa ni pamoja na kwa vyama vya ‘Ukawa’,” alisema.

Simba alisema mkutano huo utakuwa mkubwa na wa aina yake ambapo viongozi mbalimbali wa chama wanatarajiwa kushiriki na kwamba mkutano huo ratiba yake itaanza asubuhi saa tatu kwa burudani kutoka kwa wasanii mbalimbali na wananchi kuendelea kuwasili uwanjani. 
 
Sifa za Magufuli Mgombea huyo amekuwa akitajwa kuwa na sifa ya mchapakazi, makini, asiyependa uvivu, ambapo Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete alimpachika jina “Tingatinga”.

Rais Kikwete alimpachika Magufuli jina hilo, baada ya kutangazwa kuwashinda makada wengine wawili waliokuwa wakiwania kuteuliwa kuwania urais kupitia chama hicho katika Mkutano Mkuu wa chama hicho uliofanyika Dodoma.
 
 “Kila mtu anaitwa jembe lakini huyu ni zaidi ya jembe. Ni tingatinga… Magufuli ni bulldozer. Magufuli havumilii ujinga, ni mtu ambaye anataka kuona kazi zake zinafanyika kama alivyoagiza,” alikaririwa akisema.

Kikwete aliendelea kummwagia sifa Dk Magufuli kuhusu utendaji wake akisema kuwa alipokuwa akifuatilia makandarasi kwenye miradi ya ujenzi, alidiriki kuwatimua pale alipobaini walikuwa wakifanya kazi kinyume na makubaliano. 
 
Baadhi ya watu waliofanya naye kazi wamekaririwa wakisema iwapo atachaguliwa kuwa rais basi wavivu wajitayarishe kukimbia kwani Waziri huyo ni mchapa kazi wa hali ya juu.

No comments: