Sengerema.
CCM imesema kuwa itahakikisha inarudi Ikulu hata “kwa bao la mkono” wakati wa Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 25.
CCM imesema kuwa itahakikisha inarudi Ikulu hata “kwa bao la mkono” wakati wa Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika Oktoba 25.
Katibu
wa itikadi na uenezi wa chama hicho, Nape Nnauye alisema hayo katika
mkutano wa hadhara uliofanyika jana kwenye viwanja vya Nyehunge wilayani
hapa.
Neno “bao la mkono” hutumiwa kama goli
lililofungwa kwa kuupiga mpira kwa mkono kinyume cha taratibu za mpira,
lakini hukubaliwa kwa kuwa mwamuzi anakuwa hajaona kitendo hicho.
“Rangi
inayoenda Ikulu ni hii (anaonyesha shati lake la kijani ambayo hutumiwa
na chama hicho). Tuna uhakika na ushindi wa Rais. Kwa namna yoyote ile,
CCM itarudi Ikulu hata kama ni kwa bao la mkono... bao ni bao tu ili
mradi refa hajaona,” alisema Nape.
Nape, aliye kwenye
ziara ya katibu mkuu wa CCM, aliwataka wananchi wa Sengerema kusubiri
ushindi wa chama hicho na kuwakumbusha kuwa wanapaswa kuiweka CCM
kuanzia udiwani mpaka ubunge kwa nafasi ya urais tayari kuna uhakika.
Katika
mkutano huo, Nape alisema ana uhakika CCM itashinda baada ya kushuhudia
mwitikio wa Watanzania tangu alipoanza kuongozana na Kinana katika
ziara zake za kuizunguka nchi na kuzungumza na wananchi pamoja na
kusikiliza kero zao.
Amebainisha kuwa amejifunza na
kujiridhisha kuwa chama chake bado kinapendwa miongoni mwa wapigakura
waliofikiwa tofauti na vyama vya upinzani.
“Tumefika
maeneo mengi ambayo upinzani haujafika. Huko tuna hazina kubwa ya
wanachama. Hakuna namna Ukawa wanaweza kuingia Ikulu mwaka huu,”
alisisitiza.
Wapinzani waja juu
Kauli
hiyo ya Nape ilipingwa na viongozi wa vyama vya siasa vya upinzani
waliosema kuwa mtendaji huyo anamaanisha kuwa CCM itaiba kura.
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa hakutaka kabisa kuzungumzia kauli ya Nape zaidi ya kusema watakutana Oktoba.
“Kwa
bahati mbaya kauli za Nape siwezi kuzijibu. Kauli za Nape zichukue kama
zilivyo, ingekuwa ni (katibu mkuu wa CCM, Abdulraham) Kinana,
ningemjibu lakini ajue kuwa tutakutana Oktoba,” alisema Dk Slaa
alipoulizwa na Mwananchi kuhusu suala hilo.
Naibu
mkurugenzi wa habari wa CUF, Abdul Kambaya alisema kauli ya Nape
inamaanisha kuwa CCM itaiba kura kwani kwa kawaida bao la mkono ni bao
haramu.
“Kauli hiyo inaonyesha dhahiri kuwa wataiba
kura na kwa sababu katiba yetu ni mbovu matokeo yake yatatangazwa kama
yalivyo… hiyo ndiyo maana ya bao la mkono,” alisema.
Kambaya
alisema hata hivyo CCM isijiaminishe kwa lolote kwani hivi sasa
wananchi wamebadilika kimtazamo kutokana na matatizo mengi yanayoiandama
nchi kama vile afya, elimu duni na migogoro ya ardhi.
“Lakini
CCM wajue kuwa kutatokea machafuko makubwa iwapo wamejipanga kuingia
Ikulu kwa njia hiyo ya bao la mkono. Kauli ya Nape ni ya kidikteta na
inaonyesha dhahiri kuwa wamejikita kwenye utawala wa mabavu,” alisema.
Kadhalika
Kambaya alisema CUF imeshajipanga na kuhakikisha inaziba mianya yoyote
ya wizi wa kura kuanzia kwenye Daftari la Wapigakura hadi katika ujanja
wa kuwapigisha kura marehemu, askari na wanajeshi kama inavyodaiwa
kufanyika Zanzibar.
Katibu mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena
Nyambabe alisema Nape anatoa maneno ya kuvutia kwake kama njia ya
kuwakatisha tamaa wapinzani na wanachama, hata hivyo alimuonya kuwa
siasa za sasa hazitabiriki kwa njia hiyo.
“Lakini ajue
kuwa mambo yanabadilika. Anaweza kushangaa mambo yakawa mengine, sasa
hivi wananchi wana mwamko mkubwa na wanabadilika,” alisema.
Alisema
CCM haina haja ya kujitapa kwa sasa wakati bado haijapata mgombea kwani
huenda wakapata ambaye wananchi hawatamuunga mkono hata kidogo.
“Bado
CCM wana makundi jambo ambalo kwao ni udhaifu. Lakini pia lazima wajue
kuwa wakati wa mchujo utakapofika, wale watakaokatwa hawatafurahia
kuachwa na hapo kuna sababu za wapinzani kushinda,”alisema.
Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia alisema wakati Nape anabishana kwenye majukwaa, NCCR inaendelea kupiga kazi.
“Badala ya kujadili hoja za msingi zenye manufaa kwa wananchi yeye anajadili CCM kupiga bao?” alihoji Mbatia.
Akijibu
hoja ya Nape, Naibu Katibu Mkuu wa TLP, Nancy Mrikaria alisema kauli ya
kada huyo imekaa kisiasa na si kiuhalisia kwani ni kawaida kwa chama
cha siasa kujiaminisha kuwa kitashika dola.
“Unajua
chama chochote hata kiwe kidogo lazima kikiri kuwa kitashika dola ili
mradi ilani yao inakubalika na unakubaliwa na wananchi kwa sababu chama
chochote nia yake ni kuingia ikulu,” alisema.
Alisema
hata vyama vidogo kama TLP hukiri ushindi kwa kusema kuwa vinataka
kuingia ikulu kwa sababu chama hakiwezi kukiri mbele ya wananchi kuwa
hakitashinda.
Uhujumu BVR
Katika
hatua nyingine, mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Magesa Mulongo, akitoa taarifa
ya mkoa wake kwa Kinana alisema kuwa amegundua uhujumu unafanywa kwenye
mashine za kuandikisha wananchi kwenye Daftari la Wapigakura.
Alifafanua
kuwa mashine hizo za kielektroniki zinazotumika kuandikisha wapigakura
(BVR), hazina ubovu wowote na kwamba baada ya kuona kuwa kuna wakati
zinagoma kufanya kazi, huwa inakuwa kwa zote na hivyo alichukua hatua ya
kufanya uchunguzi ambao umetoa mwanga wa kinachoendelea na kwamba yupo
mbioni kuchukua hatua.
“Kuna watu hujitambulisha kama
wafanyakazi wa Tume ya Uchaguzi na kuingia ofisi za uandikishaji. Watu
hawa sijui wanafanya nini lakini huzifanya mashine zote zisifanye kazi.
Wanaingilia mfumo wake,” alisema Mulongo.
“Yupo ofisa
mmoja ambaye alichukua likizo na akaonekana sehemu ambako baadaye
mashine zilisimama kufanya kazi. Tumewapa tahadhari hiyo pia mkoa wa
Mara juu ya hujuma hii ambayo bado hatujajua inafanywa kwa maslahi ya
nani.”
Pamoja na changamoto hiyo, alifafanua kuwa zoezi
linaendelea vizuri na anatarajia kuwa lengo la kuandikisha watu 1.4
milioni litatimia kama ilivyopangwa.
Kinana anaendelea
na ziara yake ya siku 11 mkoani hapa ikiwa ni sehemu ya safari yake ya
kuizunguka mikoa ya Kanda ya Ziwa inayojumuisha pia Geita na Kagera.
No comments:
Post a Comment