Mbeya. Kazi ya Waziri Mkuu mstaafu, Frederick
Sumaye ya kusaka wadhamini juzi nusura iingie dosari baada ya wanachama
kutaka kuchana fomu zenye orodha ya wadhamini kwa madai kuwa hawakupewa
“nauli” ya kwenda ofisi za CCM kufanya kazi hiyo.
Wakati
tafrani hiyo ikitokea mjini Mbeya, Balozi Amina Salum Ali alisema mjini
Tanga kuwa hajawahi kuona nchi ambayo mtu anaiba fedha, halafu
anaambiwa azirejeshe bila ya kuchukuliwa hatua zozote, akisema huo ni
udhaifu mkubwa katika kudhibiti ufisadi.
Katika sakata
la Mbeya, kundi la baadhi ya wanachama kutoka kata nne waliokabidhi kadi
na kuandikwa majina yao kwenye ofisi za CCM za Wilaya ya Mbeya Mjini,
liliambiwa kuwa hakukuwapo na posho kwa ajili ya kazi hiyo.
Kauli hiyo ilisababisha wanachama hao kupora na kutaka kuchana fomu iliyokuwa na majina yao.
Katibu
wa CCM wilaya hiyo, Kulwa Milonge alisema tukio hilo lilikuwa kubwa na
kuhatarisha usalama, lakini chama kiliingilia kati na kusawazisha mambo.
Milonge alisema hadi mwisho wa tukio hilo, ofisa aliyetumwa na Sumaye kukusanya saini hizo aliondoka na majina 45 ya wadhamini.
Sumaye
ni mmoja kati ya wanachama wengi waliojinadi kuwa wanachukia rushwa na
ameeleza bayana kuwa iwapo CCM itampitisha mlarushwa, atajiondoa.
Balozi Amina aikomalia rushwa
Mkoani
Tanga, Balozi Amina alisema kwa kutumia uzoefu wake kimataifa katika
masuala ya fedha, amebaini kuwa kuna tatizo la kushindwa kudhibiti
ufisadi uliokithiri nchini.
“Sijapata kusikia nchi
yoyote duniani mtu anapatikana na hatia ya kufanya ubadhilifu mkubwa wa
fedha za umma, halafu anaambiwa tu arejeshe na hakuna hatua
anazochukuliwa,” alisema Balozi Amina.
Alisema iwapo
atapewa fursa ya kuwa Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano, atatumia nguvu
kubwa kupambana na ufisadi unaorutubishwa na tabia ya kulindana kwa
sababu hata kama kutakuwa na uzalishaji mkubwa, kama kuna mifereji ya
rushwa, uchumi hauwezi kukua.
Alisema Tanga ina uwezo
wa kubadilika na kuwa kitovu cha uchumi wa Tanzania nzima iwapo Bandari
ya Tanga itaboreshwa kwa kujengwa ya Mwambani na reli ya
Tanga-Arusha-Musoma hadi Uganda.
Wingi wamtisha Pinda
Wakati
mwakilishi wa Sumaye akipata matatizo hayo, hali ilikuwa tofauti kwa
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye alikuwa ofisi ya CCM ya Mbeya Vijijini
kusaka wadhamini.
Waziri Pinda alisema mbele ya
wanachama waliojitokeza kumdhamini kuwa mwili wake unasisimka na kujaa
hofu kwa jinsi wanachama wengi wanavyozidi kujitokeza kuomba urais.
Alisema anatishwa zaidi na mitazamo ya baadhi ya wagombea ambao
wanaonekana kuitaka dhamana hiyo kwa nguvu zote.
Lakini
akasema anatiwa nguvu na idadi kubwa ya wanachama wanaomuunga mkono na
kwamba anazidi kusonga mbele akimtumaini Mungu kwamba akipenda
atafanikiwa.
“Nawaomba mtuombee wote tuliojitokeza kusaka urais ili apatikane mmoja ambaye itabidi aungwe mkono na wengine wote,” alisema.
Alisema
wapo baadhi ya wagombea ambao wanaonekana kana kwamba hawatakubali
matokeo watapokataliwa na jambo hilo linaweza kuleta mtikisiko ndani ya
chama.
Lowassa adhaminiwa na maelfu
Mkoani
Mtwara, zaidi ya wanachama 3,500 walijitokeza katika ofisi za chama
hicho za wilaya kwa ajili ya kumdhamini Waziri Mkuu wa zamani, Edward
Lowassa.
“Mapokezi ya leo ni historia kubwa kwangu na
CCM, nawashukuru sana kwa sababu tangu nije Mtwara hii haijawahi kutokea
na imani huzaa imani. Hapa mmenipa Imani,” alisema Lowassa.
Alieleza sababu za kugombea akisema: “nimechoshwa na umaskini, lazima tufanye maarifa kwa uwepo wawekezaji kutoka nje.”
“Msiichezee
bahati ya gesi, uwepo wa kiwanda cha saruji, mbolea na vinginevyo
vitakavyokuja, vyote vimeshuka kwa bakuli la neema na neema hii
itaendelea kuwapo kama amani itaendelea kuwapo,” alisema.
No comments:
Post a Comment