ALI KIBA KIVUTIO KWENYE DALADALA DAR - LEKULE

Breaking

25 Jun 2015

ALI KIBA KIVUTIO KWENYE DALADALA DAR



MSANII wa muziki wa Bongo fleva hapa nchini ambaye pia ni mshindi wa tuzo za KTM 2015, Ali Kiba ameendelea kuzunguka kwenye daladala zinazofanya safari zake hapa jijini Dar es Salaam kama njia ya kuwashukuru mashabiki wake.

Mwimbaji huyo wa Chekecha cheketua alianza ziara yake hapo jana kwa kutumia usafiri wa daladala kuzunguka viunga vya jiji la Dar es Salaam akianzia kituo cha Kariakoo hadi Mbagala huku akiwalipia nauli abiria aliowakuta.
Pia alitembea na daladala kutoka Kariakoo akipitia vituo vya Magomeni, Manzese, Ubungo Simu 2000, Mwenge, Makumbusho kabla ya kumalizia Kinondoni Mkwajuni.

Akizungumza na mashabiki kwenye daladala hizo, Ali Kiba alisema aliamua kupanda daladala kwa kuamini ataweza kukutana na mashabiki wake ambao hawezi kumuona na kutoa madukuduku yao.
“Ninawashukuru kwa mapenzi yenu kwangu, bila nyinyi nisingeweza kupata tuzo hizi, nisingeweza kuwakusanya wote pamoja na kuwashukuru, nimeona kwa kutumia usafiri huu wa daladala nitaweza kuonana na baadhi ya mashabiki wa muziki wangu,” alisema.

Aliwataka mashabiki hao kumuuliza maswali au kumshauri, na alipoulizwa kama ana uhusiano wa kimapenzi na muigizaji Wema Sepetu, alikana akidai wanafanya kazi tu pamoja.

No comments: